Wananchi watakiwa kutumia ‘birthday’ zao kupanda miti

New Content Item (1)

Balozi wa mazingira nchini, Profesa Padre Aidan Msafiri, akitoa mafunzo kwa viongozi wa dini  kutoka mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara juu ya umuhimu wa utunzaji wa mazingira. Picha na Fina Lyimo

Muktasari:

  • Viongozi wa dini nchini wameshauriwa kuwahamasisha wananchi  kutumia siku za kumbukumbu zao za kuzaliwa (birthday ) kupanda  miti katika maeneo mbalimbali yanayowazunguka, kama sehemu ya zawadi zao za kukumbuka siku hiyo.

Arusha. Viongozi wa dini nchini wameshauriwa kuwahamasisha wananchi  kutumia siku za kumbukumbu zao za kuzaliwa (birthday ) kupanda  miti katika maeneo mbalimbali yanayowazunguka, kama sehemu ya zawadi zao za kukumbuka siku hiyo.

Mbali na kumbukumbu ya kuzaliwa, pia  wametakiwa kutumia siku za kumbukumbu zao za ndoa na kipaimara kupanda miti, hatua ambayo itachochea ari ya utunzaji mazingira na kudhibiti ukataji miti ovyo.

Hayo yamesemwa leo Novemba 9, 2023, wakati wakipewa mafunzo ya athari za mabadiliko ya tabia nchi yaliyokuwa yakitolewa na shirika la Kilimanjaro Consortium for Development and  Environment (KCDE) kwa kushirikina na Konrad Adenauer Stiftung (KAS) lengo likiwa ni kukabiliana na athari za mazingira ambazo zinaitesa dunia kwa sasa.

Akitoa mafunzo hayo kwa viongozi wa dini kutoka mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara, balozi wa mazingira nchini, Padri  Profesa Aidan Msafiri, amesema  viongozi wa dini wanaaminiwa na waumiwa hivyo wakitumia nafasi yao vyema swala la uharibifu wa mazingira litaweza kuthibitiwa kwa kiasi kikubwa.

Amesema katika kumbukizi za kuzaliwa, watu wamekuwa wakipewa zawadi za maua, fedha, keki na nyingine hivyo ni vyema wakajenga utamaduni wa kupanda miti  kama sehemu ya zawadi hizo na kuitunza ili kuweza kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.

"Viongozi wa dini mnaaminika kuliko watu wengine katika jamii hivyo mkitumia nafasi zenu kuna uwezekano makubwa wa kurejesha uoto wa asili na kuondokana na makali ya mabadiliko ya tabia nchi ambayo kwa sasa yanatikisa dunia," amesema

Profesa Aidan Msafiri, amesema ipo haja ya viongozi wa dini, kuanzisha klabu za mazingira na kuzishindanisha ili waumini wewe na ari ya kupanda miti hatua ambayo italeta mabadiliko.

Balozi huyo amesema, kuna haja ya kuwepo kwa utaratibu wa kutumia matamasha makubwa yanayofanyika hapa nchini, kutenga siku ya kupanda miti kabla ya kufanyika tukio husika.

Msaidizi wa Askofu Dayosisi ya Mwanga, Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Mchungaji Timothy Jonas amesema mafunzo hayo yamewapa mwanga viongozi wa dini na kupata, mbinu mpya za kuhamasisha waumini kupanda miti.

Amesema suala la kuanzisha vilabu vya mazingira ndio jambo ambalo litaenda kuleta mafinikio chanya ya kukabiliana na uharibifu wa mazingira.

Meneja Miradi Shirika la Konrad Adenauer stiftung (KAS), Damas Nderumaki amesema shirika limekuwa likiwezesha viongozi wa dini mbinu za kuhamasisha waumini  kupanda miti, pamoja na kuitunza ili kuondokana na mabadiliko ya tabia nchi.

Amesema mafunzo hayo yametolewa kwa viongozi wa dini mbalimbali 30 kutoka mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara.