Watu 87 wanusurika kifo baada ya meli ya MV Mbeya kukwama kwenye mchanga

Watu 87 wanusurika kifo baada ya meli ya MV Mbeya kukwama kwenye mchanga

Muktasari:

  • Abiria 87 wakiwepo wafanyakazi 25  wa meli ya MV Mbeya II wamenusurika kifo baada ya  meli hiyo kupigwa na mawimbi ikiwa safarini Ziwa Nyasa na kukwama kwenye mchanga karibu na Bandari ya Matema.

Mbeya. Abiria 87 wakiwepo wafanyakazi 25  wa meli ya MV Mbeya II wamenusurika kifo baada ya  meli hiyo kupigwa na mawimbi ikiwa safarini Ziwa Nyasa na kukwama kwenye mchanga karibu na Bandari ya Matema.

Akizungumza leo Jumanne Mei 4, 2021 mkuu wa Wilaya ya Kyela, Claudia Kitta ameieleza Mwananchi Digital kuwa tukio hilo limetokea jana Jumatatu Aprili 3, 2021 saa 12 jioni.

Kitta amesema kuwa awali mbali na tukio la meli hii ya abiria pia Meli ya Mizigo iliyokuwa ikitoka bandari ya Mbambay wilayani Nyasa kuja Kyela alikwama na kutitia kutokana na hali ya mawimbi katika ziwa nyasa.

"Jana saa 7 mchana tulipata taarifa ya meli ya mizigo ambayo ilibeba vifaa vya kusambaza umeme wa Rea ilititia wakati inatoka Songea kuja Bandari ya Kyela lakini wataalam walifanikiwa kuitoa na tukajua hakuna shida na ilipofika majira ya saa 12.00 jioni tukapata taarifa kwa meli yetu ya abiria kusukumwa na mawimbi na kutitia,”amesema.

Amebainisha kuwa baada ya kupata taarifa waliongozana na kamati ya ulinzi na usalama na kukuta meli hiyo ikiwa imetitia katika Bandari ya Matema.

“Ilionyesha ilisukumwa na mawimbi makali na hivyo kufanya mawasiliano wa  mamlaka husika ambao walifika na kuitoa kwenye tope, walipoichunguza hawakubaini madhara yoyote na imeendelea na safari.”

“Jana hali ya hewa ilikuwa mbaya kwani mvua ilikuwa ikinyesha upepo mkali  na mawimbi, licha ya abiria pia ilikuwa na tani 12 za mizigo, tunaendelea kuwasiliana nao kuhakikisha wamefika salama ikiwa ni pamoja na kuwaondoa hofu abiria,” amesema.