Wawili wakamatwa tuhuma za mauaji ya mwanamke gesti

Muktasari:

  • Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam limewakamata watu wawili wanaodaiwa kula njama ya kumuua mwanamke mmoja katika nyumba ya kulala wageni eneo la Tabata Segerea jijini Dar es Salaam.

  

Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam limewakamata watu wawili wanaodaiwa kula njama ya kumuua mwanamke mmoja katika nyumba ya kulala wageni eneo la Tabata Segerea jijini Dar es Salaam.

Mwanamke huyo aliyejulikana kwa jina la Barke Rashid (30) ameuawa Januari Mosi, 2022 baada ya anayedaiwa kuwa mpenzi wake White kutoa malipo ya Sh1.7 milioni kwa Jonsiner Bounser ili kutekeleza mauaji.

Taarifa iliyotolewa na Jeshi hilo leo Jumanne Januari 25, 2022 imeeleza kuwa chanzo cha maauaji hayo ni mwanamke huyo kukabwa shingo mpaka kupoteza maisha akiwa katika nyumba hiyo ya wageni.

“Inadaiwa mtuhumiwa wa kwanza alikodiwa na mtuhumiwa wa pili kwa malipo ya Sh1.7 milioni ili amtongoze na baadae aende kumuua mwanamke huyo kwa madai kuwa mtuhumiwa wa pili alimgharamia sana na kumpangishia nyumba lakini ilidaiwa na mtuhumiwa wa pili kuwa mwanamke huyo ana wanaume wengine.

“Mtuhumiwa wa kwanza amekiri kupewa  Sh1.2  kwa nyakati tofauti kabla na baada ya kutekeleza mauaji hayo na kwamba alikuwa bado anadai Sh500,000  kwa mtuhumiwa wa pili kwa mauaji ya mwanamke huyo, uchunguzi wa tukio hilo unakamilishwa na watafikishwa Mahakamani haraka iwezekanavyo” imeeleza taarifa hiyo.