Waziri Makamba atoa wiki mbili kumaliza tatizo la umeme
Muktasari:
- Waziri wa Nishati, January Makamba ametoa wiki mbili kuhakikisha hakuna tatizo la kukatika umeme nchini endapo likitokea wahusika watachukuliwa hatua.
Dar es Salaam. Waziri wa Nishati, January Makamba ametoa wiki mbili kuhakikisha hakuna tatizo la kukatika umeme nchini Tanzania.
Leo Ijumaa Septemba 17, 2021 Makamba amefanya ziara ya kushtukiza katika ofisi za Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) baada ya malalamiko ya wananchi kuongezeka kuhusu kukatika kwa umeme .
Makamba amesema atakayeshindwa kutekeleza majukumu yake na malalamiko ya kukatika kwa umeme yakiendelea kujitokeza, wahusika wote watachukuliwa hatua.
"Ndani ya wiki mbili sitaki kusikia kukatika kwa umeme nikisikia kuna malalamiko nitachukua hatua Kwa wahusika walioshindwa kutekeleza wajibu wao," alisema Makamba.
Alisema wanahitaji Shirika hilo lijiendeshe kibiashara, kisasa ambapo mabadiliko yenye tija yataongeza ufanisi na mapato yataongezeka.
"Shirika lina wateja wa mita 3.2 milioni wanakusanya zaidi ya Sh2 tirioni na hakuna Shirika lolote hapa nchini linalotengeneza fedha hizo, hivyo wateja wanatakiwa kuongezeka ili Shirika liweze kujiendesha" amesema
Naye Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Uzalishaji wa Umeme, Pakaya Mtimakaya amesema wameyapokea maagizo hayo na watayafanyia kazi.