Haya hapa madhara ya kuchelewa kuanza kliniki

Mwanamke anapopata ujauzito huwa na mawazo ni lini hasa anatakiwa aanze kuhudhuria kliniki ya afya ya uzazi.

Kwani wengi wao hawafahamu ni lini ndiyo muda muafaka wa kuanza kuhudhuria kliniki na wengi wao huchelewa kuanza kupata huduma hiyo.

Lakini wataalamu wa afya wanatuambia kliniki ya afya ya uzazi kwa mjamzito ni pale tu anapogundua kuwa ni mjamzito.

Wanasema ni vizuri hata kabla mwanamke hajashika ujauzito yeye na mwenzi wake wanaweza kuanza kuhudhuria kliniki.

Hii ni njia nyepesi inayoweza kuwafanya wazoee kuhudhuria kliniki hata wakati wa ujauzito.

Kliniki ya afya ya uzazi si kliniki ya wanawake pekee bali hata wanaume inawahusu.

Mara zote inashauriwa mjamzito anapoanza kliniki anatakiwa aende mwenza wake. Kuanza kliniki mapema kuna faida ikilinganishwa na mjamzito anayechelewa kuanza.

Kwani akiwahi kutamsaidia kupata huduma stahiki mapema na kuchelewa huweza kusababisha kukosa baadhi ya huduma katika kipindi cha ujauzito.

Naijulikane kwamba kuhudhuria kliniki wakati wa ujauzito kuna umuhimu mkubwa maana hili jambo limekuwa mara nyingine likichukuliwa kama ni la kawaida na halitiliwi mkazo na watu wengi.

Mahudhurio hafifu au kutohudhuria kliniki kunaweza kusababisha matatizo kwa mtoto au mama kabla au wakati wa kujifungua.

Kwanini jambo hili linatiliwa mkazo

Upimaji na matibabu ya maradhi ya zinaa, yakiwamo ya klamidia kisonono, kaswende, trikomonasi, UkimwiI na homa ya ini hupewa kipaumbele kutokana madhara yanayoweza kumkumba mama au mtoto katika kipindi cha ujauzitoa au wakati na baada ya kujifungua.

Maambukizi ya maradhi kama Ukimwi kama mjamzito atakuwa nayo, humsababishia mfumo wa kinga mwilini mwake dhidi ya maradhi kuwa hafifu.

Hali hali hiyo humuweka mjamzito katika hatari ya kushambuliwa na maradhi mbalimbali nyemelezi yanayoweza kuathiri ujauzito wake.

Pia utambuzi wa maambukizi ya VVU husaidia wauguzi kupanga namna sahihi ya kumzalisha mjamzito huyo ili kuepusha maambukizi kwa mtoto.

Kisonono hushambulia mfumo wa uzazi na mkojo.

Hali hii husababisha mfereji wa mkojo kuziba.

Mara nyingi mtoto huambukizwa ugonjwa huu mama anapojifungua na humsababishia mtoto kuugua maradhi ya meno.

Kaswende huwa na tabia ya kusambaa sehemu nyingine za mwili kama kwenye moyo na mifupa.

Na kama utashambulia mfumo wa fahamu, unaweza kusababisha homa ya uti wa mgongo inayoitwa kwa jina la kitaalamu meningitisi na hata mtoto aliyeko ndani ya mfuko wa uzazi anaweza pia asiumbike kikamilifu au anaweza kupoteza maisha.

Trikomatisi husababisha kupasuka kwa chupa mapema na kumfanya mjamzito ajifungue katika muda usio sahihi au mama anaweza kujifungua mtoto njiti.

Klamidia unaweza kusababisha uvimbe kwenye fupa nyonga, hivyo kuharibu tishu zinazohusiana na uzazi.

Hali hiyo humsababishia matatizo mjamzito hata wakati wa kujifungua na mara nyingine humsababishia kifo.

Kwa upande wa mtoto inaweza kumsababishia maambukizi kwenye njia ya hewa hasa kwenye mapafu na huweza pia kumsababishia upofu kama macho yatashambuliwa.

Mardhi ya Malaria kipindi cha ujauzito yanaweza kusababisha kujifungua kabla ya muda na huweza kusababisha mimba kutoka, maradhi ya anemia sugu, maradhi kwenye kondo la nyuma, kujifungua mtoto njiti, hivyo kumuweka katika hatari ya kupoteza maisha ndani ya siku 28 baada ya kuzaliwa.

Hivyo, ni muhimu kwa mjamzito kutumia chandarua chenye dawa wakati wa ujauzito na kuhudhuria kliniki kwa ajili ya kupatiwa dawa za kinga dhidi ya malaria.

Je tetenasi nayo inamadhara gani?

Tetenasi ni moja ya maradhi yanayoongoza kwa kusababisha vifo kwa wajamzito na watoto wachanga hasa katika nchi zinazoendelea. Hivyo, ni muhimu kukamilisha chanjo yake.

Kipindi cha ujauzito kuna uhitaji mkubwa wa damu katika mwili wa mjamzito ili kukidhi mahitaji ya mama na mtoto.

Kwa kutambua umuhimu huo, wajawazito hupatiwa dawa kwa ajili ya kuongeza kiwango cha damu kila waendapo kliniki.

Pia hupatiwa dawa za minyoo ili kuzuia maradhi ya kuhara. Mardahi hayo husababisha upungufu wa maji na damu kama mjamzito ataugua.

Maradhi mengine hatarishi ni UTI. Mama akienda kiliniki hupimwa na akigundulika kuugua, hupatiwa matibabu mapema kwa sababu yanaweza kusababisha mimba ikatoka au kujifungua mtoto njiti.

Kuhudhuria kliniki husadia pia kutambua maendeleo ya ukuaji wa mtoto aliyeko tumboni.

Kama una maswali wasiliana na Dk Kammu kwa simu namba 0759 775788