Siyo kila uvimbe kwenye mfuko wa uzazi ni saratani

Dk Christopher  Peterson

Muktasari:

  • Lakini wataalamu wa afya wanasema si kila uvimbe hutokana na ugonjwa wa saratani, bali mwingine husababishwa na mambo mengine, ila haupaswi kupuuzwa kwani huenda ukawa na madhara ya aina nyingine kwenye mfuko wa uzazi.

Ni dhahiri kuwa moja ya dalili ya saratani huambata na uvimbe kwenye sehemu husika ya mwili kulingana na aina yake. Dhana hii imezua hofu miongoni mwa wanawake wengi, hasa inapotokea baada ya vipimo kugundulika kuwa wana uvimbe kwenye mifuko yao ya uzazi.

Lakini wataalamu wa afya wanasema si kila uvimbe hutokana na ugonjwa wa saratani, bali mwingine husababishwa na mambo mengine, ila haupaswi kupuuzwa kwani huenda ukawa na madhara ya aina nyingine kwenye mfuko wa uzazi.

Kuna uvimbe unaoitwa kitaalamu uterine fibroids, huu hautokani na saratani na mara nyingi huota na kukua kwenye ukuta au tabaka lililopo kwenye mfuko wa uzazi.

Uvimbe huo hautofautiana kwa ukubwa wa maumbile na wakati mwingine ukicheleweshwa unaweza kukukua kwa ukubwa wa tikiti maji.

Pia, hautofautiana kwa idadi kati ya uliomuota mwanamke mmoja na mwingine, kwani mmoja unaweza ukaota zaidi ya mmoja kwenye mfuko wake wa uzazi, lakini mwanamke mwingine unaweza ukaota mmoja tu.

Mara nyingi uvimbe unaota mmoja, madhara pindi unapokuwa na kuonezeka, huukandamiza mfuko wa uzazi na kuulazimisha upanuke hadi kugusa kwenye viwambo vya mbavu, hapo ndipo matatizo mengine yanapoanza.

Wanawake wengi wanakuwa hupatwa na uvimbe huu, lakini hawatambui kama wanao kwa sababu mara nyingi hauonyeshi dalili hadi pale unapokuwa mkubwa kupita kiasi na kuanza kuleta matatizo kiafya.

Hivyo, wanawake wanawashauri kujenga utamaduni wa kupima mara kwa mara ili kuubaini kabla ya haujaleta madhara makubwa.

Kama nilivyoeleza hapo juu, uvimbe huu huchukua muda hadi kuanza kuonyesha dalili zake, lakini kama mtu ana utamaduni kupima mara kwa mara anaweza kubaini dalili zake ambazo ni pamoja na kupata hedhi iliyopitiliza. Hali hiyo inaweza kusababisha mtu kupata anemia, maumivu ya mgongo na kiuno, haja kubwa kwa shida, maumivu makali chini ya kitovu na hasa ikitokea uvimbe umeshakuwa mkubwa.

Pia anaweza akawa anaenda haja ndogo mara kwa mara kuliko kawaida na kujisikia maumivu makali wakati wa tendo la ndoa.

Ukiona dalili hizo, ni dhahiri una tatizo hilo na ni vema kwenda hospitali kwa ajili ya vipimo na mpango wa matibabu.

Uvimbe unaoota kwenye mfuko wa uzazi japo hauwezi kusababisha saratani, lakini una madhara mengine makubwa kiafya.

Madhara hayo ni pamoja na matatizo wakati wa kujifungua, yanaweza kuhatarisha maisha ya mama na mtoto kama mama alishika ujauzito wakati tayari ana huo uvimbe. Lakini, unaweza pia kusababisha kutobeba ujauzito au kutungwa nje mfuko wa uzazi na tatizo lingine kubwa, ni mimba kuharibika mara kwa mara.

Sababu kubwa zinazochangia tatizo hili ni matatizo yanayojitokeza kwenye mfumo wa homoni. kisayansi, kwenye mwili wa mwanamke kuna homoni (vichocheo) za estrogen na progesterone. Homoni hizi mbili zinafanya kazi ya kuchochea maendeleo ya ukuaji wa sehemu ya ndani ya mfuko wa uzazi kwenye kila mzunguko wa hedhi wa kila mwezi, kwa ajili ya maandalizi ya urutubishwaji wa mayai na utungishwaji wa mimba, sasa wakati mwingine huwa inatokea homoni hizo hujichochea zaidi ya kiwango hivyo kuanza kutengeneza uvimbe mdogo mdogo kwenye ukuta wa mfuko wa uzazi.

Lakini pia tatizo hili linahusishwa na sababu za kurithi. Ni vema kwa mwanamke kuijua vizuri historia ya ukoo wake ili kutambua kama naye yupo kwenye hatari ya kurithi ugonjwa huo au la!

Kwa sababu mara nyingi mtu anaweza kuupata ugonjwa huo kupitia vinasaba vitokavyo kwa watangulizi wake wa ukoo. Sababu zingine zinazochangia kwa kiasi kikubwa tatizo hilo ni pamoja na kupata hedhi katika umri mdogo, matumizi ya baadhi ya njia za uzazi wa mpango, uzito wa mkubwa wa mwili, ukosefu wa vitamin D na ulevi pia.