Ney wa Mitego: Kuvuta jiko?…bado sana

Ney wa Mitego

Muktasari:

Awalinyota wa muziki nchini na barani Afrika, Diamond Platnumz aliwahi kunukuliwa mwaka jana akisema kuwa hawezi kumuoa mchumba wake wa zamani, Wema Sepetu, kauli ambayo baadaye aliikanusha.

Huenda ile dhana kwamba wasanii wanaogopa kuoa kwa sababu wanahisi watashuka chati, inaweza ikawa na ukweli ndani yake, kwa mujibu wa msanii nyota wa hiphop nchini, Ney wa Mitego.

Awalinyota wa muziki nchini na barani Afrika, Diamond Platnumz aliwahi kunukuliwa mwaka jana akisema kuwa hawezi kumuoa mchumba wake wa zamani, Wema Sepetu, kauli ambayo baadaye aliikanusha.

Lakini Ney wa Mitego, ambaye kwa sasa ana mtoto wa kiume aliyempata kwa mchumba wake, Siwema Oktoba mwaka jana, ameamua kufunguka akieleza bayana kuwa hana mpango wa kuoa kwa sasa mpaka akamilishe baadhi ya mambo.

“Sijasema kwamba siwezi kuoa, ila kwa sasa siwezi kulizungumzia suala hilo. Kuna vitu nakamilisha na vikiwa tayari watu wote watajua,” alisema rapa huyo. “Ni kweli kwamba Siwema ni mchumba wangu ninayempenda sana na nashkuru amenizalia mtoto ila mipango yetu ni baadaye.”

Alipoulizwa kuhusu idadi ya watoto alionao na iwapo ana mpango wa kumhalalisha Siwema au mwanamke mwingine kati ya watatu aliozaa nao, Ney alisema:

“Nina watoto wengi, ila kifupi nitakwambia kwamba ninao watatu na kati ya hawa kila mmoja ana mama yake. Sasa siwezi kulisemea hili moja kwa moja. Maisha ni duara hujui wapi utagota, lakini niseme tu kwamba nampenda sana Siwema.”

Ney wa Mitego, ambaye anasema anamiliki nyumba yenye thamani ya Sh180 milioni, alisisitiza kuwa bado hajamaliza baadhi ya mambo yake katika muziki, hivyo ni vigumu kuingia kwenye majukumu ya ndoa kwa sasa.

Hata hivyo picha alizozitupia katika mitandao wiki hii, zinamwonyesha akiwa amevaa pete inayoonekana kuwa ya ndoa, lakini alipoulizwa alikuwa na jibu jingine.

“Hahaahaaa pete hii naivaa huu mwaka wa sita sasa, tangu nilipopewa zawadi na rafiki yangu anayeishi nje ya nchi. Hii ni zawadi na lazima niitunze kwa kuwa kwanza ninaipenda,” alisema.

Anasema mwonekano alionao hivi sasa ndiyo unaofanya vitu vitu vingi ambavyo watu hawakuwahi kuvichunguza, vionekane.

“Mwonekano wangu mpya kwa sasa ndiyo umewafanya wengi kunichunguza na kuiona hii pete. Ukweli ni kwamba si ya ndoa na sijaoa bado, ila watambue kwamba mwaka huu nimejipanga kivingine. Kuna mambo mengi ambayo nitayafanya kupitia muziki,” alisema.

“Miaka ya nyuma nilikuwa mtu ambaye sijachangamka sana katika fani. Sasa nataka kwenda kisasa na nifanye kazi ya muziki kivingine kabisa. Nilikuwa hata video zangu nafanya ndani ya nchi nikitoka nje ni Kenya nimerudi tena ndani, ila mwaka huu nabadilika na ndiyo maana unaniona suti kali nini, mambo yanabadilika sasa,” anasema.

Ney wa Mitego anasema licha ya mipango hiyo amefanya ‘kolabo’ mbili nje ya nchi na anatarajia kufanya video na watayarishaji wakubwa ili kuitangaza nchi kimataifa kupitia muziki wa hiphop.

“Taratibu zinaendelea nimefanya kolabo na wasanii wa nje nyimbo mbili zipo tayari, moja nimefanya na msanii kutoka Nigeria na nyingine ni msanii wa Ghana na zipo mwishoni kukamilika.

Nipo tayari kufanya kolabo na msanii yeyote kutoka nje ili kusukuma muziki wangu mbali zaidi na kuitangaza nchi, hivyo watu watarajie ngoma moja kali kutoka kwangu na kolabo nyingine za kimataifa zitakazosindikizwa na video kali,” anasema rapa huyo.