Mafumu nguli wa ‘midomo ya bata’

Mafumu Bilal katikati akipuliza Saxophone

Muktasari:

  • Akiwa darasa la sita ndipo alipobaini kuwa anapenda muziki kwani alikuwa akimwona mjomba wake mwanamuziki Shem Kalenga Mkurugenzi wa Tabora Jazz, akipiga gitaa la besi katika bendi ya Lake Jazz.

Ni moja ya wanamuziki wenye kipaji cha pekee katika upulizaji wa mdomo wa bata, maarufu Saxephone, pamoja na umahiri katika chombo hicho, lakini pia ni mpigaji mzuri wa gitaa la solo na rhythm, kama hiyo haitoshi ni mwimbaji mzuri licha ya kuchelewa kugundua kipaji hicho.

Alianza rasmi kujiingiza kwenye muziki mwaka 1973, lakini hadi leo ni moto wa kuotea mbali kutokana na kuwa maahiri wa kufanya kazi hiyo ambayo kwa mujibu wake atakufa akiifanya.

Hapa namzungumzia mmiliki wa Bendi ya African Beat, Mafumu Bilal Bombenga ‘almaarufu Super Sax’, alifanya mahojiano na gazeti hili nyumbani kweke Vingunguti Kiembe Mbuzi, ili kujua au kusikia kutoka kwake alianza lini muziki na kwa nini yupo hapo alipo sasa.

Mafumu alianza kueleza safari yake ya muziki ilivyoanza kwa kusema kuwa kama siyo moyo wa dhati wa kupenda muziki wala asingefika hapo alipo kwa kuwa baba yake mzazi aliyekuwa mganga maarufu mkoani Kigoma, Mzee Bilali hakutaka kabisa awe mwanamuziki kwa kuhakikisha kila akijaribu kujiingiza kwenye masuala hayo anamtoa.

“Mzee Bilal hakutaka kabisa kusikia muziki alipenda nisome sana dini, lakini nilikuwa kila nikipata nafasi hata kwa kuchana uwa natoroka na kwenda kwenye muziki,” alianza kueleza historia yake ya muziki.

Mafumu anasema kuwa alizaliwa mwaka 1958, Mwanga-Kigoma, Barabara ya Legeza Mwendo, na kupata elimu ya msingi katika shule ya H.H Aga Khan, kabla ya kuhamia Tabora ambapo alisoma elimu ya sekondari katika Shule ya Kazima.

Anasema akiwa darasa la sita ndipo alipobaini kuwa anapenda muziki kwani alikuwa akimwona mjomba wake mwanamuziki Shem Kalenga, Mkurugenzi wa Tabora Jazz, akipiga gitaa la besi katika bendi ya Lake Jazz.

“Nilidhamiria moyoni kuwa nitakuwa kama mjomba licha ya kuwa na vikwazo kutoka kwa baba aliyekuwa hapendi kabisa mambo hayo, nilikuwa nakwenda anakopiga kwa kupasua ua kwa kuwa ulikuwa wa nyasi na kurudisha kama ulivyokuwa na nilikuwa nikifanya hivyo mara nyingi,” anasema Mafumu.

Anaeleza kuwa siku moja aliamua kuchonga ubao akaweka na kopo la mafuta ‘dumu’ na nyuzi za kuvulia samaki ‘mshipi’ akapata gitaa la solo la kienyeji, lililokuwa linamfanya anakuwa bize kiasi cha kutosikia hata mtu akiongea pembeni yake hadi amguse.

“Sikufundishwa na mtu nilijifunza kupiga gitaa kwa kuangalia hasa nilikuwa naweza kukaa hata saa namwangalia mjomba akipiga na mwisho nikajua bila kuelekezwa kushika wala kuambiwa hiyo ni nyuzi hii fanya hivi wala nini,” anasema Mafumu.

Anaendelea kueleza kuwa baadaye alikuwa akienda kwenye bendi ya Kigoma Jazz kwa kutoroka, ili azidi kuongeza ujuzi kwa kuangalia na wengine wanapiga kama mjomba wake au laa, na kukuta ujuzi unazidiana na kutofautiana lakini taratibu ni zilezile.

Anasema alijifunza kupiga Saxephone, alipokuwa Kazima Sekondari ambapo alichaguliwa kuwa mmoja wa wanaopiga Blassband, “nilijiachia na kupiga vifaa vingi lakini nikanufaika zaidi kwani niliweza kupuliza sax na hapo umahiri ndiyo ulipoanza,” anasema.

Anasema baada ya kumaliza shule alikwenda Makutupora Dodoma jeshini kwa mujibu wa Sheria na mwaka 1973, yakatangazwa majina ya waajiriwa la kwake halikuwepo lakini aliambiwa asubiri orodha nyingine, hata hivyo akaamua kutoroka kwenda Morogoro kwenye bendi ya Morogoro Jazz.

“Nilikwenda kujiunga na Moro Jazz bila kuwa na ndugu katika mji huo, yaani nilikwenda moja kwa moja kwenye bendi na nikapokewa wakati huo ndio hayati Mbaraka Mwinshehe anaondoka kwenda kuunda bendi yake ya Super Volcano,” anasema Mafumu.

Anasema hakukaa sana na bendi hiyo kwani alikuta ndiyo inaelekea mwisho baada ya kuondoka kwa Mwinshehe, akaja Dar kwa kaka yake na kujiunga na bendi ya Western Jazz waliokuwa wakitumia mtindo wa ’saboso’ ikiwa chini ya uongozi wa Shamba Ramadhani.

Anautaja mshahara wake wa kwanza kupokea akiwa na bendi ya Western ni Sh.275, ambazo alizitumia zote kununua nguo.

“Nilikuwa naishi kwa kaka yangu kila kitu bure na nilikuwa napenda sana kuvaa, hivyo nikautumia mshara wote kununulia nguo wakati huo sikuwa mnene kama leo nilinunua suruali za mtindo wa bugaluu, viatu vya raizoni na mashati ya kubana ya kutosha kwa kuwa ndiyo nilianza kuona umuhimu wa kuwa mwanamuziki na jinsi gani natakiwa kung’aa,” anasema Mafumu huku akicheka.

Anaeleza kuwa wakati huo hakuwa akiimba bali alikuwa anapuliza mdomo wa bata na kupiga rhythm gitaa.

Anasema akiwa Western wapinzani wao wakuu walikuwa ni bendi ya Dar Jazz ‘majini wa bahari’ ambapo pamoja na muziki bendi hizi pia zilikuwa ni wapinzani wa jadi katika soka kwani Western Jazz ilikuwa ni Yanga ingawa yeye hashabikii timu hiyo na Dar Jazz ni Simba, hivyo bendi hizo zilijigawa katika mtindo huo na ilikuwa marufuku na haikutokea Western kupiga kwenye tafrija za Simba na Dar Jazz vile vile kwenye za Yanga.

“Mamluki kama mimi wasiokuwa wanachama au mashabiki wa timu inayoshabikiwa na bendi husika walikuwepo lakini mashabiki na wapenzi wa bendi hizi walijigawa katika mtindo huo Western Yanga na Dar Jazz Simba, ilikuwa wenyewe huwaambii kitu hasa mtajiri wa Western na ushabiki wa soka wa zamani ulikuwa wa kweli,”anafafanua Mafumu.

Anazitaja nyimbo ambazo zilitamba wakati yupo na bendi hiyo kuwa ni pamoja na jela ya mapenzi, Rosa, Vigelegele na Hakika, huku akiutaja ukumbi mkuu wa bendi hiyo kuwa ni Community Centre uliokuwepo ilipo sasa Makao Makuu ya Wilaya ya Kinondoni, maeneo ya Magomeni Mapipa.

Itaendelea wiki ijayo ambapo Mafumu atataja bendi nyingine ambazo aliwahi kufanya nazo kazi na nyimbo zilizokuwa zikitamba, alipata wapi jina la Supersax, na ilikuwaje akaanza kuimba.