Kwa ripoti hii ya CAG, Rahis anzisha ‘lifestyle audit’

Nkwazi Mhango

Mpendwa Rahisi, sorry, Raisa, nisikuzeeshe kukuita mama, tunakaribiana kiumri. Usijali lugha yangu. Tatizo ni ufyatu. Dhiki zimenifyatua hadi nafyatuka, kuchanganyikiwa, kuchanganyika huku nikichanganya mambo.

Muhimu, nakuheshimia sana dada yangu. Naomba sikio. Kwa unyenyekevu, nifyatuke. Iko makini soma ripoti ya Kaguji, Zibiti Juluku ya Sirkal (KAZIJUSI kama jusi nabanwa na lango) au Covering Addiction and Greed (CAG). Yeye danganya nani?

Ile juluku ya Fatu, sirkal haina dukani vala sambani. Ripoti imenivuruga, imeniharibia siku yangu. Imeniachia machungu na huzuni. Kila mwaka, ripoti ikitolewa ni ufyatuaji mabilioni kwenda mbele utadhani sirkal ni kipofu au taahira. Heri muifiche mtuondelee maumivu. Naomba univumilie. Tatizo ni wafyatuaji au wale wanaopaswa kuwafyatua wapigaji?

Una mamlaka kikatiba na vyombo vya kunusanusa kama Takokuru hata geshi. Lalinda nini kama tunapigwa hivi? Kila mwaka, tunapigwa utadhani hatupo! Tatizo nani na nini? Hivi vyombo vya nini au mapambo?

Niepuke mgongano kimaslahi. Mie si chawa wala mpingaji. Sisifu, kuimba mashairi wala mapambio. Ni Fyatu Mfyatuzi mzalendo wa kupigiwa mfano anayechukia rushwa, uchawa, ufisadi, na upigaji njuluku za mafyatu waliochoka kufyatuliwa na shida wakati majizi yakipiga njuluku ndefu yakiishi peponi. Pia, huchukia kuona mamlaka zikiangalia utadhani hazipo.

Leo sifyatui mengi wala magumu. Niliwahi kumwandikia mtangulizi wako bingwa wa kutumbua namna ya kukomesha huu mchezo mchafu. Hakunijibu wala kufanyia kazi ushauri wangu. Naamini. Naambiwa u msikilizaji mzuri, unanisikia? Utafanyia kazi mwarobaini huu ninaotoa bure.

Nashauri uanzishe utaratibu wa kukagua na kujiripoti kwa watumishi wote wa umma, kuwachunguza ndugu/washirika wao (Kimakunduuchi, lifestyle audit). Tuna mapanya na wezi wengi wakwasi wakubwa. Tunawajua. Unawajua. Wanajijua.

Fyatu kamaliza shule juzijuzi. Kaajiriwa Bandari, Takokuru, Uhamiaji, Benki Kuu, Viwanda, Uhamiaji, Polisi, Mahakama, nk. kwenye mshiko, ni bilionea ghafla bin vu bila maelezo! Waulize mafyatu. Watakutajia wezi wote. Wanaishi nao. Wanawajua.
Wanawaona. Haihitaji PhD katika udukuzi/upelelezi. Ukiona nyuso zao, utawajua.
Tunga sheria kukagua, kuchunguza hata kushuku mali zinazoonekana wazi kupatikana kipigaji.

Ipe meno. Taifisha na tupilia lupango wahusika, kuondoa mazingira na motisha vinavyowawezesha hawa panyabuku kutufyatua na kutupiga. Amini. Mafyatu watakupenda. Watakusaidia.

Wamegeuza kaya shamba la bibi kipofu na taahira tukishuhudia upigaji mabilioni ilhali unavuja jasho kwenda ughaibuni kubomu au kuvutia wawekezaji ili panyabuku wachache wabukue na kufyatua. Ukishindwa, useme wazi tuwaulize mafyatu wenye kaya la kufanya.

Pili, tafadhali anza kufyatua. Ukichelea kutumbua au kuogopa usaha licha ya historia ya kutumika vibaya huko nyuma, useme. Mfano, zikitolewa au kuripotiwa tuhuma za wizi, weka kando wahusika ili wachunguzwe.

Juzijuzi, zilitokea tuhuma kuwa akina Riz One wanapiga njuluku Mirerani. Nini umefanya pamoja na vyombo vya habari kufichua hujuma hii?

Tatu, unda taasisi ya siri kuwachunguza Takokuru wanaowachunguza wengine kieleweke, isiwe tunacheza kamchezo ka kuajiri ngedere kulinda ndizi tukijua wanavyozipenda. Ikibidi wape geshi. Huko Kenya, watumishi wengi wa umma weshashikwa na kunyang’anywa mali zote walizoshindwa kuzitolea maelezo au zilizopatikana kifisadi.

Nne, kama muarobain huu haufai wala huna dhamira ya kisiasa kuzifanyia kazi, utangaze kaya yetu iitwe Fyatuliwa kieleweke. Maana, inasikitisha na kuchukiza sina mfano, kushuhudia mafyatu wakijituma kuzalisha na kutengeneza utajiri unaopigwa na kufyatuliwa na mafyatu wachache wasio na uzalendo wala uaminifu.

Sisteri, naamini. Kama utaanzisha lifestyle audit na kuhoji mali walizo nazo watumishi wa umma, utashinda kansa hii licha ya kukinukisha na kukiumanisha. Pia, haitakuwa mara ya kwanza kuleta mapinduzi katika kupambana na ufisi na ufisadi. Awamu ya Mzee Mchonga mwana wa Burito (RIP sana) ilisifika kwa kunusanusa na kupambana na ufisi, ufisadi, na upigaji wa njuluku za mafyatu.

Wakati ule, naamini ulikuwa mkubwa, ukipiga ulabu kupita kiasi au kuuramba sana, unabanwa na kueleza unapopata hiyo njuluku ya matanuzi wakati mafyatu wakitanuliwa na kufyatuliwa na ufukara wa kutengenezwa na ngurumbili.
Unda chombo cha kupokea malalamiko ya rushwa na ulimbikizaji mali mafyatu watakupa kila kitu.

Ukishawanasa wezi, hakikisha, kabla ya kuwadaka na kuwafilisi, unatunga sheria kali ili kila kitu kifanyike kisheria na kisayansi tusiishie kuwatengenezea wao na mawakili wao ulaji utokanao na kushinda kesi mahakamani.

Sheria itamke wazi kuwa kaya ina mamlaka kisheria kutaifisha fedha na mali za wizi.
Nashauri tutumie msamiati wa kurejesha mali za umma badala ya kutaifisha ili wajanja uchwara wasiwatishe wawekezaji kuwa tunarejea kwenye zama za ujima na ujamaa za kutaifishana.

Kumalizia, anza operesheni hii na watumishi wa Takokuru na taasisi nyingine zenye ushawashi kifedha. Amini.

Nakwambia. Siku moja utanitafuta na kunishukuru kwa uzalendo na ubunifu. Nimaliza kwa heshima na taadhima bila kufyatuka. Asante sana dada yangu na karibu ufyatuni.