Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Sababu Baraza la mawaziri Equatorial Guinea kujiuzulu

Rais wa Equatorial Guinea, Teodoro Obiang 

Muktasari:

  • Rais Obiang asikitishwa na utendaji duni, rushwa na kushindwa kuimarisha uchumi

Malabo. Baraza la mawaziri la Serikali ya Equatorial Guinea limejiuzulu baada ya kushindwa kutekeleza malengo ya maendeleo iliyokuwa imepewa tangu ilipoteuliwa mwaka 2024, hatua inayotafsiriwa kama pigo kubwa kwa utawala wa taifa hilo linalotegemea kwa kiasi kikubwa sekta ya mafuta na gesi.

Tangazo hilo limetolewa leo na Makamu wa Rais wa nchi hiyo, Teodoro Mangue, ambaye pia ni mtoto wa Rais Teodoro Mbasogo.

Amesema Waziri Mkuu, Manuel Osa Nsue Nsua, amewasilisha rasmi barua ya kujiuzulu kwa niaba ya mawaziri wote wa Serikali kutokana na tathmini iliyoonyesha kuwa Serikali hiyo ilifanikiwa kutekeleza chini ya asilimia 10 ya malengo iliyokuwa imewekewa.

Makamu huyo wa Rais amesema hatua hiyo imechukuliwa kwa kuzingatia kanuni ya uwajibikaji katika utumishi wa umma, akisisitiza kuwa viongozi wa Serikali wanapaswa kuwajibika pale matokeo ya kazi zao yanaposhindwa kufikia matarajio ya wananchi.

"Uwajibikaji katika usimamizi wa shughuli za umma lazima uambatane na matokeo. Kiwango cha utekelezaji kilichofikiwa ni kidogo sana ukilinganisha na matarajio na ahadi zilizotolewa," amesema kupitia ujumbe wake kwenye mtandao wa X.


Rais Obiang akerwa na rushwa na matumizi mabaya ya rasilimali

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na chama tawala cha Democratic Party of Equatorial Guinea (PDGE), Rais Obiang ameridhika kuwa Serikali iliyomaliza muda wake haikuweza kutekeleza majukumu yake kwa kiwango kilichotarajiwa.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa Rais alibaini kuwepo kwa vitendo vya rushwa, matumizi mabaya ya rasilimali za Serikali kwa maslahi binafsi pamoja na kushindwa kusimamia kikamilifu utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyokuwa imepangwa.

Aidha, Serikali hiyo imelaumiwa kwa kusuasua katika utekelezaji wa sera za kiuchumi zilizolenga kupunguza utegemezi wa taifa hilo kwenye mafuta na gesi.

Chama hicho kimesema Rais Obiang alionesha kutoridhishwa na ukweli kwamba juhudi za kuimarisha sekta nyingine za uzalishaji, hususan kilimo, hazikupewa kipaumbele cha kutosha licha ya umuhimu wake katika kuimarisha usalama wa chakula na kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje.


Serikali yashindwa kuondoa utegemezi wa mafuta

Miongoni mwa hoja kuu zilizochangia kujiuzulu kwa Serikali hiyo ni kushindwa kuendeleza mpango wa muda mrefu wa kuibadilisha uchumi wa Equatorial Guinea kutoka utegemezi mkubwa wa mafuta kwenda katika sekta nyingine zenye uwezo wa kuzalisha ajira na mapato endelevu.

Kwa miaka mingi, Equatorial Guinea imekuwa ikitegemea mafuta kama mhimili mkuu wa uchumi wake. Sekta ya mafuta na gesi inachangia sehemu kubwa ya mapato ya Serikali pamoja na mauzo ya bidhaa nje ya nchi.

Hata hivyo, kupungua kwa uzalishaji wa mafuta na kushuka kwa mahitaji ya bidhaa hiyo katika soko la dunia katika miaka ya karibuni kumeathiri vibaya uchumi wa taifa hilo.

Matokeo yake, ukuaji wa uchumi umedorora, mapato ya Serikali yamepungua na uwezo wa kufadhili miradi ya maendeleo umeendelea kukabiliwa na changamoto.


Utajiri wa mafuta haujanufaisha wananchi wengi

Licha ya Equatorial Guinea kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mafuta barani Afrika na kuwa na mapato makubwa kutokana na rasilimali hizo, wananchi wengi wa taifa hilo lenye takribani watu milioni 1.8 bado wanaendelea kuishi katika mazingira ya umaskini.

Ripoti mbalimbali za maendeleo zimekuwa zikionesha tofauti kubwa kati ya utajiri wa taifa na hali halisi ya maisha ya wananchi, huku huduma za kijamii na fursa za kiuchumi zikiendelea kuwa changamoto kwa sehemu kubwa ya jamii.

Wachambuzi wa uchumi wanaeleza kuwa utegemezi mkubwa wa mafuta, ukosefu wa utofauti wa vyanzo vya mapato pamoja na changamoto za uwajibikaji katika matumizi ya rasilimali za umma ni baadhi ya sababu zinazochangia hali hiyo.


Obiang aendelea kutawala kwa zaidi ya miongo minne

Hatua ya kuvunjwa kwa Serikali imekuja wakati Rais Teodoro Obiang Nguema Mbasogo akiendelea kushikilia rekodi ya kuwa kiongozi aliyekaa madarakani kwa muda mrefu zaidi duniani.

Obiang amekuwa Rais wa Equatorial Guinea tangu mwaka 1979 baada ya kuchukua madaraka kupitia mapinduzi ya kijeshi.

Katika kipindi chote cha utawala wake, amedumisha ushawishi mkubwa wa kisiasa huku akiwateua watu wa familia yake kushika nafasi mbalimbali muhimu serikalini.

Miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa katika utawala huo ni Makamu wa Rais Teodoro Nguema Obiang Mangue, ambaye kwa muda mrefu ametajwa kuwa mmoja wa warithi wanaotarajiwa kuendelea na uongozi wa taifa hilo siku zijazo.


Serikali mpya yasubiriwa

Baada ya kujiuzulu kwa Serikali yote, macho ya wananchi na wadau wa siasa yanaelekezwa kwa Rais Obiang ambaye anatarajiwa kutangaza Baraza jipya la Mawaziri katika siku zijazo.

Serikali mpya itakabiliwa na jukumu kubwa la kurejesha imani ya wananchi, kuimarisha uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma, kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuandaa mikakati madhubuti ya kuimarisha uchumi usiotegemea mafuta pekee.

Hatua hiyo pia inakuja wakati Equatorial Guinea ikitafuta njia za kukabiliana na changamoto za kiuchumi zinazotokana na mabadiliko ya soko la nishati duniani, huku wananchi wakitarajia kuona maboresho ya maisha yao kupitia matumizi bora ya utajiri wa mafuta na gesi ambao taifa hilo limejaaliwa kuwa nao.