Aliyegombea ubunge asakwa na Polisi

Aliyekua mgombea  wa ubunge  kupitia CHADEMA,Rogers Ruhega

Muktasari:

Pia jeshi la polisi linayashikilia magari matatu yaliyokuwa yakitumiwa na mgombea huyo kwenye kampeni kwa tuhuma za kukutwa yakiwa na silaha mbalimbali kama mapanga,sime na fimbo kinyume cha sheria.

Geita. Jeshi la Polisi mkoani Geita linamtafuta aliyekua mgombea  wa ubunge  kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Rogers Ruhega kwa tuhuma za kuhusika na shambulio la kudhuru mwili  wa Moshi Paul akiwa na vijana wengine 25.

Pia jeshi la polisi linayashikilia magari matatu yaliyokuwa yakitumiwa na mgombea huyo kwenye kampeni kwa tuhuma za kukutwa yakiwa na silaha mbalimbali kama mapanga,sime na fimbo kinyume cha sheria.

Kamanda wa polisi mkoani Geita Mponjoli Mwabulambo alikiri kukamatwa  kwa magari hayo na kusema yalikamatwa yakiwa na silaha hizo  usiku wa kuamkia oktoba 25 majira ya saa sita usiku.

Akizungumzia malalamiko yaliyotolewa na Mke wa aliyekuwa mgombea Golda Ruhega kulilalamikia jeshi la polisi kufika nyumbani kwake usiku wakiwa na silaha na kuitisha familia Kamanda Mwabulambo alisema polisi wanafanya kazi kwa mujibu wa sheria.

“polisi kufika nyumbani kwake ni kwa mujibu wa sheria na kama yeye ni mtu mzuri ajiulize kwa nini polisi wafike nyumbani kwake usiku ni vyema akajisalimisha mwenyewe badala ya kusubiri kukamatwa na polisi”alisema Kamanada.

Alisema Rogers anahusishwa na tukio la shambulio na kukutwa na silaha kinyume cha sheria na kumtaka kujisalimisha polisi badala ya familia yake kulalamika kwenye vyombo vya habari

Awali mke wa aliyekuwa mgombea akizungumza na waandishi wa habari alidai kundi la askari  zaidi ya saba wa jeshi la polisi wamekuwa wakifika nyumbani kwake usiku wa manane wakiwa na silaha amilia yake.

“mimi nashindwa kuwaelewa hawa polisi kwa sababu siku hawa vijana wanakamatwa hata mume wangu alikuwepo sijui kwa nini waliwakamata hao vijana wakamuacha yeye alafu sasa ndio wanasumbua “

Mwanamke huyo alidai kitendo kilichofanywa na polisi kukamata magari ya mume wake na kumzuia kupeleka barua za mawakala ni sababu moja wapo iliyochangia mume wake kushindwa katika kinyanganyiro cha ubunge katika jimbo la Geita mjini.

Katika uchaguzi uliofanyika oktoba 25 mwaka huu katika jimbo la Geita mjini ilihusisha wagombea watatu katika nafasi ya ubunge ambapo Kanyasu John aliibuka mshindi kwa kupata kura 34,953 sawa na 55% Rogers Ruhega alipata kura  26,303 sawa na 41.5 % na Malebo Michael alipata kura 625 sawa na 0.1%