Arsenal, Man City vita bado ngumu

VITA ya ubingwa ndani ya Ligi Kuu England imeendelea kuwa tamu, hiyo ni baada ya Arsenal na Manchester City zote kushinda mechi zao leo huku tofauti ya pointi ikiwa ni moja tu kileleni kwenye msimamo wa ligi hiyo.

Arsenal ilipata ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Tottenham na kufikisha alama 80, huku Man City ikiichapa Nottingham Forest na kufikisha pointi 79.

Hata hivyo, Man City ina faida ya mchezo mmoja mkononi ikiwa imecheza mechi 34 na Arsenal 35, hivyo ikishinda mchezo wao wa kiporo itakuwa imekaa juu ya Washika Mitutu hao kwa tofauti ya pointi mbili.

Mchuano unaonekana kuwa mkali baina ya timu hizi wakati huu ambapo ligi inaelekea ukingoni zikiwa zimebakia mechi tatu kwa Arsenal kabla ya kumaliza msimu huku Man City ikibakiwa na nne.

Timu yoyote kati yao itakayoangusha pointi ama kwa sare au kwa kufungwa itajikua imejiweka kwenye mazingira magumu zaidi ya kuchukua ubingwa.

Man City inatazamia kuchukua taji lake la nne mfululizo ambapo itakuwa imeweka rekodi yakuwa timu ya kwanza kufanya hivyo katika historia ya Ligi Kuu England.

Katika mechi ya Arsenal iliyopigwa London Stadium mabao yao matatu yalifungwa kipindi cha kwanza kupitia kwa Pierre Emile Hojberg, aliyejifunga, Bukayo Saka na Kai Havertz huku, Spurs yenyewe ilifunga kipindi cha pili kupitia kwa Christian Romero na Son Heung Min, aliyefunga kwa mkwaju wa penalti.

Man City iliyopata ushindi wa mabao 2-0, moja lilifungwa na beki wao Josko Gvardioli kisha lapili likafungwa na Erling Haaland, ambaye sasa amefikisha mabao 21 na hivyo kujiweka sawa kwenye mbio za kuwania Kiatu cha Dhahabu cha ligi hiyo msimu huu, akimzidi kwa bao moja staa wa Chelsea, Cole Palmer.

MECHI ZILIZOBAKIA KWA MAN CITY

Wolves (Nyumbani)

Fulham (Ugenini)

Tottenham (Ugenini)

West Ham (Nyumbani)


MECHI ZILIZOBAKIA KWA ARSENAL

Bournemouth (Nyumbani)

Man United (Ugenini)

Everton (Nyumbani)