Dk Ndumbaro azitabiria Simba, Yanga kukutana CAFCL

Muktasari:

  • Timu ya Simba itacheza mechi ya ufunguzi dhidi ya Al Ahly ya Misri mchezo wa Ligi ya African Footbal Jumamosi wiki hii kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Damas Ndumbaro amesema hatua ambayo Simba na Yanga zimefikia kucheza makundi Ligi ya Mabingwa Afrika huenda ikatokea timu hizo siku moja zikakutana na kushuhudiwa dabi yao ya kimataifa.

 Dk Ndumbaro amesema hayo leo Oktoba 16, 2023 alipotembelea ofisi za Baraza la Kiswahili la Taifa (Bakita) na kuzungumza na watumishi wa taasisi hiyo.

“Itakuwaje siku moja Simba na Yanga zinakutana katika mechi ya Ligi ya Mabingwa, hiyo dabi itakuwaje, amehoji Waziri Dk Ndumbaro.

Amesema ni matumini makubwa ya Serikali kuona timu mbili zinazishiriki michuano ya Ligi ya African Football mwakani.

Amesema iwapo tu timu hizo zikifanikiwa katika mashindano ya mwaka huu kufika hatua ya robo fainali, kuna uwezekano tukawa na timu mbili Ligi ya Mabingwa Afrika na Ligi ya African Football mwakani.

“Hatua ya CAF kuamua mechi ya ufunguzi wa Ligi ya African Football kufanyika nchini, ni heshima kubwa kwa Taifa, na hiyo yote ni kutokana na dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassan kuendeleza michezo.

Pia, amesema hatua hiyo italinufaisha Taifa kiuchumi kwani vijana ambao watapata nafasi ya kutumbuiza katika ufunguzi watajipatia 'maokoto'.

Dk Ndumbaro amesema Tanzania inajivunia mafanikio ya michezo chini ya Rais Samia kwa kuwezesha timu ya kwanza ya wanawake kucheza Kombe la Dunia, vilevile hatua nzuri iliyofikia timu ya wanawake ikiwa hatua moja kuelekea kufuzu Afcon ya wanawake.

Akizungumza kuhusu nafasi ya Kiswahili katika michezo, Katibu Mtendaji wa Bakita, Consolata Mushi amesema baraza hilo litaendelea kusambaza kamusi na machapisho mbalimbali ili kuwafikia watu mbalimbali waweze kuzungumza Kiswahili sanifu hata katika michezo.

Amesema baraza hilo lipo tayari kushirikiana na wanamichezo ili kuhakikisha iwapo wanakutana na ugumu wowote wanalitatua tatizo kwa pamoja.