Mayele, Bangala wapiga mkwara Yanga

Muktasari:

  • Yanga msimu huu inataka rekodi tu, baada ya kuvuka makundi kwa mara ya kwanza kwenda robo fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika, sasa mastaa wa timu hiyo wamepiga mkwara na kutamba kuwa, wanataka heshima mbele TP Mazembe watakaovaana nao Aprili 2 kukamilisha mechi za makundi.

Dar es Saalam. Yanga msimu huu inataka rekodi tu, baada ya kuvuka makundi kwa mara ya kwanza kwenda robo fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika, sasa mastaa wa timu hiyo wamepiga mkwara na kutamba kuwa, wanataka heshima mbele TP Mazembe watakaovaana nao Aprili 2 kukamilisha mechi za makundi.

Timu hizo zipo Kundi D na katika mchezo wa kwanza baina yao, vinara wa kundi hilo na wa Ligi Kuu Bara, ilishinda nyumbani kwa mabao 3-1 na sasa zitakutana kwenye mechi ya kufungia hesabu ambapo mastaa wa Yanga walisema iwe isiwe ni lazima washinde kwa lengo la kuweka heshima yao.

Mechi hiyo inatarajiwa kupigwa jijini Lubumbashi na kama Yanga itashinda tena na matokeo ya Monastir itakayoikaribisha Real Bamako ya Mali itaisha kwa sare ya wenyeji kupoteza, itamaanisha Yanga itamaliza kinara na Watunisia kusalia nafasi ya pili kama ilivyo kwa sasa zote zikifuzu robo.

Licha ya kila mchezaji wa Yanga kuitaka kwa hamu mechi hiyo, lakini kuna mastaa sita raia wa DR Congo, Joyce Lomalisa, Djuma Shaban, Fiston Mayele, Yanick Bangala, Tuisila Kisinda na Jesus Moloko wanaokiwasha Jangwani wameikamia mechi hiyo wakitamba wanataka kuweka heshima.

Sababu kuu ya mastaa hao kuwa na uchu na mechi hiyo ni kutokana na wengi wao kuwahi kupita AS Vita katika nyakati tofauti ambao ni wapinzani wa jadi na Mazembe nchini DR Congo  hivyo wanataka kuonyesha ukubwa wao kwa wapinzani hao wa muda mrefu.

Licha ya kuwa tayari Yanga imeshakata tiketi ya kucheza robo fainali ikiongoza kundi D na alama 10 sawa na Monastir ya Tunisia tofauti ikiwa mabao ya kufunga na kufungwa lakini mastaa hao wamesema hawajamalizana na Mazembe kwani wanataka washinde nyumbani na ugenini.

Mshambuliaji Fiston Mayele mwenye mabao matatu hadi sasa kwenye michuano hiyo alisema wanahitaji ushindi kwenye ardhi yao ya nyumbani ili kuonyesha ubora wa na Yanga kwa ujumla.

"TP Mazembe ni timu kubwa DR Congo lakini na Yanga ni kubwa kwa Tanzania, sasa tunataka kushinda mechi hii ili kuonyesha ukubwa wa Yanga katika michuano ya kimataifa," alisema Mayele aliye kwenye kikosi cha timu ya taifa ya DR Congo na kuongeza;

"Haiutakuwa mechi nyepesi lakini tumejipanga kushinda na kumaliza hatua ya makundi tukiongoza kundi."
Winga Jesus Moloko mwenye mabao mawili alisema ushindi dhidi ya Mazembe utawaheshimisha mastaa hao ambao wamekuja Bongo kupiga kazi.

"DR Congo ni nyumbani kwetu lakini sisi tunacheza Tanzania siku hizi. Ni maisha ya mpira na tupo hapa kuipambania Yanga ili kufikia malengo na kuweka heshima," alisema Moloko kwa niaba ya Wakangomani wenzake.

Yanga imeendelea kujifua kwa mechi hiyo kabla ya kusafiri kwenda Lubumbashi siku ya Machi 30  kuvaana naMazembe huku ikiwa imeweka mkakati wa kuambatana na mashabiki watakaokuwa tayari kusafiri na basi la timu hiyo kwa kulipa sh 700,000.

Ikirudi baada ya mechi hiyo, Yanga itakabiliwa na mechi mbili ngumu ikiwamo ya robo fainali ya Kombe la ASFC dhidi ya Geita Gold itakayopigwa Aprili 8 na siku chache itaikaribisha Kagera Sugar kwenye pambano la Ligi Kuu Bara.

MECHI ZIJAZO APRIL  02, 2023
Yanga v TP Mazembe (CAF-ugenini)

Aprili 08, 2023
Yanga v Geita Gold (ASFC-nyumbani)

Aprili 11, 2023
Yanga v Kagera Sugar (Ligi-nyumbani)

Aprili 16, 2023
Yanga v Simba (Ligi-ugenini)