Bunge la Ndugai ‘limeuza’ mamlaka yake Ikulu

Muktasari:

Kanuni zilizozoeleka za Bunge siku hizi zinawashangaza hata wabunge wenyewe. Hii ni kutokana na mambo yanavyoamuliwa kulingana na tukio

 

Hivi karibuni niliandika makala nikijadili utendaji wa Spika wa Bunge, Job Ndugai. Nilisema katika makala hayo na naendelea kusisitiza kuwa Spika huyu ama ameshindwa kuyatambua mamlaka ya Bunge analoliongoza au anaogopa kuyatumia na kuishia kuiachia Serikali anayotakiwa kuisimamia.

Madaraka ya Bunge yanaelezwa katika ibara ya 63(2), ikisema:  “Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri  ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa

majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii.”

 

Leo nitaangazia madaraka hayo ya Bunge katika uundwaji wa kamati teule. Kanuni za Bunge ibara ya 120 fasili ya 1 na 2 zinasema, “Kamati Teule inaweza kuundwa na Bunge kwa madhumuni maalumu kwa hoja mahsusi itakayotolewa na kuafikiwa. Baada ya kujadili hoja yoyote, Bunge linaweza kuunda Kamati Teule

kwa madhumuni ya kushughulikia jambo lolote lililotokana na hoja.”

Julai 5, Spika Ndugai aliunda kamati maalum ya Bunge kwa ajili ya kutathimini uchimbaji, usimamizi, umiliki na umiliki na udhibiti wa madini ya almasi nchini, kisha kuandaa mapendekezo mahsusi kwa ajili ya kuishauri Serikali juu ya uendeshaji wa biashara ya madini hayo.

 

Hadidu za rejea kwa kamati hiyo iliyoongozwa na Mbunge wa Ilala, Mussa Zungu zilikuwa pamoja na kuchunguza hadidu za rejea za kamati zilizoundwa awali zilizochunguza uchimbaji na udhibiti na kuona kama zinaweza kuhuishwa kwa matumizi ya sasa.

 

Nyingine ni kuchunguza mfumo wa usimamizi wa biashara ya almasi nchini na kuanisha manufaa na hasara ambayo Serikali kutegemea na uwekezaji uliopo.

 

Ya tatu ni kupendekeza mfumo bora unaoweza kutumika katika kusimamia uchimbaji na uwekezaji na kushughulikia jambo lolote linalohusiana na biashara ya almasi.

Kamati hiyo iliyopewa siku 30 kutekeleza majukumu yake iliwasilisha matokeo yake Septemba 7 bungeni Dodoma.

Tatizo sasa linapokuja na ndiyo hoja yangu kwa leo ni kitendo cha Spika mara tu baada ya kuipopokea, kumkabidhi makabrasha ya ripoti ya kamati hiyo pamoja na kamati ya kuchunguza madini ya Tanzanite Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye naye alizipeleka Ikulu kwa Rais John Magufuli.

Kanuni za Kudumu za Bunge ibara ya 122 na fasili za 2 na 3 zinasema, “Taarifa ya Kamati Teule itawasilishwa Bungeni na Mwenyekiti. Iwapo baada ya hoja kutolewa, Bunge litaamua kujadili taarifa hiyo, hoja itakayotolewa Bungeni itakuwa ni kwa madhumuni ya kuliomba Bunge likubali mapendekezo yaliyomo katika taarifa hiyo.”

 

Katika mchakato mzima hatukuona Spika akiwauliza wabunge kama kuna haja ya kujadili ripoti zile. Badala yake sherehe zilifanyika nje ya ukumbi wa Bunge aqmbapo ripoti zilikabidhiwa kutoka kwenye kamati husika kwenda kwa Spika ambaye naye alizikabidhi kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

 

Sina uhakika, kama Spika Ndugai mwenyewe alipata muda wa kuzisoma ripoti zenyewe au alikwenda kusikia zikisomwa mbele ya Rais Ikulu ya Dar es Salaam.

 

Najiuliza tu, Spika Ndugai alikuwa na haraka gani ya kupeleka ripoti hizo Ikulu? Je, alilazimishwa? Alitishwa?

 

Mbona uzoefu unaonyesha ripoti ya kamati teule za Bunge kusoma ripoti zake bungeni na zikajadiliwa na mapendekezo yalitolewa? Mfano mzuri ni kamati teul;e ya Bunge iliyochunguza mradi wa umeme tata wa Richmond mwaka 2007.

Kamati hiyo iliyoundwa na Spika Samuel Sitta iliongozwa na Waziri wa Habari wa sasa Dk Harrison Mwakyembe, ilileta taarifa yake bungeni, ikadiliwa na hatimaye aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa alijiuzulu.

Uzoefu pia umeonyesha ripoti za Serikali zimekuwa zikiletwa Bungeni na kujadiliwa kisha Bunge linaielekeza Serikali cha kufanya.

 

Tuliona kwa mfano, ripoti ya Operesheni tokomeza iliyotokana na tume iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete na kujadiliwa bungeni.

Tunaona pia ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) zikijadiliwa bungeni, licha ya kukabidhiwa kwa Rais.

 

Kinachofanyika sasa kwenye Bunge la Spika Ndugai ni kinyume, kamati anaiunda yeye mwenyewe, lakini matokeo yake yanakwenda kusomwa Ikulu.

 

Hata mpishi huonja kwanza chakula kabla hakijaenda mezani kwa walaji, kwa hiyo Ndugai naye kama mpishi wa ripoti hiyo alipaswa kuisoma na kuwaruhusu wabunge wachangie kabla ya kuipeleka Serikalini.

 

Tulitarajia kuona madudu yaliyomo kwenye ripoti hizo yakijadiliwa bungeni na wabunge watoe mapendekezo. Kwa mfano, katika ripoti hiyo kamati ilieleza kubaini, miaka ya nyuma kuna kiongozi mkubwa alipewa zawadi ya Almasi yenye thamani ya Dola za Marekani (USD) milioni 200 sawa na Sh400 bilioni za Tanzania.

 

Kiongozi huyo ni nani? Je, ni Rais mstaafu? Au ni mungu mtu? Haya yote yangebainika bungeni, lakini ni aibu kuona unge likizibwa mdomo na Spika anaridhia, madudu ya kamati hizo yanafunikwa kwa visingizio lukuki.

 

Pengine Rais Magufuli alikuwa na malengo yake ya kutaka ripoti hizo zikasomwe Ikulu moja kwa moja, lakini Spika Ndugai naye alipaswa kusimamia madaraka yake ya Bunge.

 

Lengo siyo ushindani bali ni kutekeleza madaraka yake kama mhimili mmojawapo wa Serikali. Kila mhimili una madaraka yake na haipaswi kuingiliana.

 

Ni kwa msingi huo tunaona jinsi Bunge linavyomong’onyolewa katika awamu hii ya tano. Walianza kukataza Bunge lisionyeshwe moja kwa moja katika televisheni, tumeona hata wabunge wakikatazwa kuwajadili marais wastaafu na sasa ripoti za Bunge zinakwenda kusomewa Ikulu.

Bunge kwa sasa limebakiza nini tena? Spika Ndugai na viongozi wenzake wamebakiza nini? Iko wapi dhana ya Bunge kuisimamia Serikali?