Dakika 10 za uso kwa uso na Future

Muktasari:

  • Future ni msanii ambaye kwa sasa anawika zaidi duniani kote na mtindo wa kurap kwa kuzungumza maarufu kama Trap. Mtindo ambao baada yake kumekuwa na wasanii wengi wameamua kufanya muziki kwa namna hiyo kiasi kwamba sasa Future anaonekana kama ndiye muanzilishi.

Rapa wa Marekani, Future atatua Bongo mwaka huu na kutumbuiza Julai 22 katika viwanja vya Leaders Club jijini Dar es Salaam.

Future ni msanii ambaye kwa sasa anawika zaidi duniani kote na mtindo wa kurap kwa kuzungumza maarufu kama Trap. Mtindo ambao baada yake kumekuwa na wasanii wengi wameamua kufanya muziki kwa namna hiyo kiasi kwamba sasa Future anaonekana kama ndiye muanzilishi.

Mtandao wa E ulifanya mahojiano katika kipindi cha Ten Minute With a Star na haya yalikuwa mazungumzo yao:

Wakati unaandaa albamu yako ya Hendrix hukuwa ukiposti picha kwenye mitandao ya kijamii wala ukiandika chochote kwa ajili ya mashabiki wako. Inadaiwa uliachana na matumizi ya mitandao kipindi hicho. Je, hili lina ukweli.

Ni kweli, nilifanya hivyo kwa sababu nilikuwa nahitaji muda wa kutosha kwa ajili ya kufikiria mambo mengine, kufikiria cha kuandika katika nyimbo zangu na kufikiria jinsi ya kufanya kitu kipya na bora.

Unajua, mitandao ya kijamii ni mizuri lakini inatafuna muda mwingi, unapotaka ku-post picha ni lazima utumie muda kuipiga na kuandika ‘caption’, kabla picha haijaenda kwenye mtandao. Kwa hiyo niliamua kupumzika.

Kama mtumiaji mzuri wa mitandao ya kijamii. Ulijisikiaje kuacha kuitumia kwa muda?

Kwangu ilikuwa ni kitu kizuri kwa sababu sikuwa nikihitajika kumjibu yeyote aliyeandika kitu kuhusu mimi, wala sikuwa nikihitaji kuandaa kitu chochote kwa ajili ya kuzungumza na mashabiki wangu. Zaidi nilikuwa napata muda mwingi wa kuwa studio, muda mwingi wa kuwa na watoto wangu na familia kwa ujumla.

Kwa nini umeamua kuiita albamu yako jina la msanii mwingine?

Unamzungumzia Hendrix sio? Ni kwa sababu namkubali Jimi Hendrix, napenda alichokuwa anakifanya enzi za uhai wake, alikuwa ni nyota ingawa watu wa asili yake (weusi) hawakutaka kukubaliana na hili.

Na hicho ni kitu kinachonifanya nijione kama tunafanana hivi kwa sababu naamini nafanya vitu vikubwa, ila kuna watu hawataki kukubaliana na mimi, wengine wanadai nimeuharibu muziki kabisa kwa hiki ninachokifanya.

Ni msanii gani ambaye huwa unamsikiliza sana?

Mimi huwa simsikilizi msanii yeyote, huwa najifunza muziki tu. Na huwa najifunza kupitia kusikiliza muziki mzuri uliofanikiwa kibiashara bila kuangalia ni nani aliyeimba. Nasikiliza mistari, midundo, melodi na kila kitu?

Nini malengo yako kwa siku za usoni?

Nimepanga kuacha kila kitu kuhusu muziki katika siku za usoni, nitakuwa nafanya mambo binafsi tu. Na ndio maana kwa kipindi hiki najitahidi sana kufanya kazi kwa bidii ili muda wa kuachana na muziki ukifika niwe nilishajenga msingi imara na niweze kusimama kiuchumi.