NDANI YA BOKSI: Dar es salaam bila King Kong...

Aboubakar Shaaban Katwila muite Chilla. Kama Chid Benz asingekaza yangetokea yale ya Jaffaray na wimbo wake wa ‘My Boo’. Chilla asingekubali kiitikio chache kielee elee juu ya mistari ya hovyo na vocal mbovu. ‘”Muda” bonge la wazo. Bonge la biti. Bonge la muunganiko wa sauti laini na ngumu. Kifupi ni ngoma lililotendewa haki. Wimbo usingekamilika bila Chilla na wazo la wimbo “Muda” lisingekuwa na maana kama lingeimbwa na mtu mwingine badala ya Chid Benz.

Katika wasanii ambao Diamond anamtazama kwa jicho la tofauti ni Chilla. Naamini anatamani pepo limtokee adondokee pale WCB kinuke tu. Kina Tekno na Pana wake wangejuta. Q Chilla ni tatizo sana.  Fundi. Yule ndiye picha  sahihi ya fleva za Kibongo. Wakati mwingine mtu unajiuliza amekwama wapi? Usipate jibu, na ukikutana naye akakueleza ya nyuma ya pazia unaishia kumuombea Mungu. Kamsikilize kwenye kiitikio cha wimbo wa Chid “Muda” unaweza kudhani ni msanii mpya maana zile kelele zilizounganishwa na midundo ambazo ndiyo nyingi kwa sasa huwezi kuzipata kwenye kinywa na kichwa cha Chilla.

Timing mbovu na mikwamo inayoleta stress kwa wanamuziki wengi ndo chanzo cha basi walilopanda kina Christian Bella na wenzake limuache njiani Chilla.

Bila hivyo wasingepata upenyo kibwegebwege na ‘kushaini’ kirahisi tu. Wangefanya kazi maana unapotoa kitu unamtazama aliye mbele yako. Mbele yako kuna Chilla utatoaje wimbo wa hovyo  ili utoboe?

Chilla leo hii anaingia kwenye jukwaa la wasanii ambao ni wakali kuliko ukali wenyewe lakini hawapati kile wanachostahili. Kamsikilize kwenye “Muda” maneno machache anayarudiarudia tu mtu unatamani angemaliza wimbo wote peke yake. Bahati nzuri kakutana na mtoto wa kihuni toka mitaa ya Ilala mwenye sauti yenye mamlaka na mitambao ya haja.

Hakutaka kuachwa na ladha ya Chilla katambaa naye na kuufanya wimbo kuwa wimbo na siyo jingo.

Kilichofanyika kwa Chilla na Benz ni muendelezo wa wanamuziki wa kitambo kile, kuamua kufanya kazi badala ya lawama nyingi na chuki kwa watoto wa sasa ambao wanakimbiza kama wamerogwa.

Umemsikiliza Mteule Jaymoe katika “Nisaidie Kushare”? Ni ngoma ya tani nyingi sana kuanzia ‘biti’ michano na kile anachoongelea. Yule ndiye Jaymoe halisi ambaye alitoweka kwenye “Pesa Madafu”. Wengine wanashindwa nini? Ni maswali ya watu wengi sana ambao wapo maofisini kwa sasa na kipindi kile walikuwa mashabiki wao wakiwa mashuleni.

Kuna ‘testi’ ya game ilitoweka hapo katikati kutokana na mafuriko ya staili za Kinijeria. Na wanamuziki wengi wakakaa kando kwa kushindwa kwenda na kasi iliyopo na wengine kuelemewa na matumizi ya dawa za kulevya na wengi wao ni stress tu.

Wenye stress wengi wao walijikuta wako kando ya game baada ya kukorifishana na wasimamizi wao. Bushoke katoweka kwa namna hiyo, siyo kuishiwa mashairi wala kukosa studio.

Utajiri wa sauti na uwezo wa kuandika wa Chilla ni mtaji mkubwa sana. Anachokosa ni akili ya kujiongeza iliyopo kwenye ubongo wa mtu mmoja tu kwa sasa ambaye ni Diamond. Chilla siyo kwamba kakosa usimamizi bali kakosa hata kujua tu nani anastahili kumsimamia.  Siku ubongo wake utakapoamka na kujua afanye nini na nani kwa njia ipi. Kuna watu watakimbia mji.

Jamaa mkali sana ni wale wanamuziki ambao wanaweza kuigeuza njano kuwa bluu kwa usiku mmoja.

Kasikilize wimbo wa “Taabasamu” wa Mr Blue achana na michano ya Blue na kiitikio cha Steve R&B. Kasikilize mwishoni kabisa mwa wimbo Chilla kavuruga kila kitu. Kaonyesha yeye ni nani na Steve RnB ni nani. Fundi sana na wengine watakuja kujua balaa lake mpaka siku atangulie mbele za haki. Lakini kwa sasa ni madini yanayozurula tu mitaa ya jiji la Dar we Salaam, badala ya kupishana na kina Davido kwenye maviwanja ya ndege na ‘kuselfika’ na watoto wazuri kwenye majukwaa makubwa nje ya mipaka ya Bongo.

Chilla ni madini kuliko wengi wanavyodhani. Bila ubora wa Chid Benz. Bila mitambao amazing ya KING KONG. Bila kukaza sauti na kujipindua kwa swaga kama za kwenye Jahazi na G Habashi baaaasi... yangemtokea ya Mteule Jafaray.

Miaka ya nyuma Chilla alitengeneza kiitikio cha wimbo wa “My Boo” wa Jafaray. Wakapishana kiswahili kidoogo. Chilla akabeba kiitikio chake na kuongeza maneno machache tu. Dunga amkanyongea ‘biti’ akaingiza  sauti na kuacha wimbo ujisambaze wenyewe. Ukawa mwisho wa wimbo wa Jafaray siyo kwa kutopigwa redioni bali kwa kutosikilizwa hata ukipigwa. Chilla fundi.

Kumsikiliza Chilla katika wimbo Subuhi wa  AY na FA ni zaidi ya kupokea nyongeza ya mshahara katika utawala wa Magu. Anaimba kama hataki. Hatari sana Chilla.