Mo Rashid yuko darasani Simba

Muktasari:

  • Mshambuliaji huyo amejiunga na Simba akitokea Prisons msimu huu

Dar es Salaam. Mshambuliaji mpya wa Simba, Mohamed Rashid anazidi kuendelea kuona vikubwa ndani ya kikosi hicho baada ya kukiri kwamba maandalizi yao kuelekea msimu mpya wa 2018/19 ni makubwa tofauti na alikotoka Prisons.

Mo Rashid amesema namna ambavyo matajiri wa timu hiyo wanavyopanga mikakati ya namna watakavyotetea ubingwa na kumtaka kila mchezaji atambue wajibu wake na kujua kwa nini yupo kwenye timu.

"Naendelea kujifunza vitu vingi vinavyonibadilisha mtazamo, kuona naweza nikafika mbali zaidi, kikubwa natakiwa kujituma na kujitunza mwili wangu kuwa tayari kwa ajili ya majukumu.

"Nimeamini kweli Simba ni klabu kubwa, unajua hata inakuamsha mchezaji kuwaza vitu vikubwa kutokana na jinsi ambavyo mabosi wanavyotazama mbali na kuwa na melngo makubwa," alisema Rashid.

Mohamed anasema anaamini msimu ujao kwake utakuwa na manufaa yatakayotokana na ushindani wa kuwania namba mbele  ya wakongwe wanaoamini ndani ya kikosi hicho.

"Ushindani unamfanya mchezaji kuwa bora kwani kila wakati anakuwa anaboresha kiwango chake akiogopa kupiga benchi, unajua tofauti na pale unapoona wewe ndiye tegemeo la kwanza," alisema Mo Rashid.