Unavyoweza kukabiliana na hofu kabla ya kupima afya

Wakazi wa kisiwa cha Juma kilichopo wilayani Ukerewe mkoani Mwanza wakiwa kwenye foleni kwa ajili ya kuchunguzwa afya zao na kupewa matibabu bure kisiwani hapo juzi, matibabu hayo yalitolewa na Shirika la Christian Life World Mission Frontiers la Nchini Korea. Picha na Maktaba

Muktasari:

  • Licha ya kuwapo kwa elimu na jitihada kubwa za Serikali na mashirika mbalimbali kuhusiana na vita dhidi ya ugonjwa huo, bado kuna ukakasi mkubwa kwa mtu kufanya uamuzi wa kujitokeza kupima afya ili kujua usalama wao ukoje.

Tangu ugonjwa wa Ukimwi ulipogundulika, licha ya kusababisha vifo vya maelfu ya watu, umendelea kuibua hofu kwa watu na miongoni mwa vitu vinavyoogopwa sana kuhusu ugonjwa huo ni suala la kupima afya ilikubaini kama mtu anamaambukizi ama laa.

Licha ya kuwapo kwa elimu na jitihada kubwa za Serikali na mashirika mbalimbali kuhusiana na vita dhidi ya ugonjwa huo, bado kuna ukakasi mkubwa kwa mtu kufanya uamuzi wa kujitokeza kupima afya ili kujua usalama wao ukoje.

Kama kunasababu kubwa inayosababisha vita dhidi ya ugonjwa huo kuwa ngumu ni pamoja na suala la watu kutofanya uamuzi wa kupima afya zao ili taratibu nyingine za kiafya ziweze kufuata.

Lakini wataalamu wa saikolojia wanasema kadiri mtu anavyokuwa na uelewa wa jambo fulani kwa kina, ndivyo hofi nayo hutoweka.

Kwa maana hiyo, watu ambao wanahofu ya kupima afya zao au kukimbia majibu baada ya kupima virusi vya ukimwi, hawajaelewa vizuri umuhimu wa kupambana na ugonjwa huo kwa manufaa ya kizazi kilichopo na kijacho.

Umuhimu wa kujua afya yako

Kuna faida lukuki za mtu kutambua afya yake kwani njia pekee ya kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi mapya ya ugonjwa wa Ukimwi kwa upande wa kuambukiza au kuambukizwa, ni mtu kujitambua yupo upande gani.

Kuzuia maambukizi mapya, kupima afya na kuchukua majibu yako, kunamuwezesha mtu kubadili mfumo wa maisha yake. Kwani akishatambua hauna maambukizi, kwa vyovyote atakua makini katika kujilinda aidha kwa kuwa mwangalifu sanjari nakupunguza mambo hatarishi.

Pia, itamsaidia kama anamaambukizi ya virusi amkinge mwenzake na yeye pia asipate maambukizi mapya yanyoweza kinga zake za mwili kushambuliwa kwa kasi zaidi.

Watu wanaamini kupima afya ilikujua upande waliopo ni jambo la kuogofya, lakini ukweli kukaa bila kujua afya yako ni jambo la kutisha zaidi kuliko kujitambua kuwa tayari una maambukizi.

Kwani mtu akishajitambua atachukua tahadhari kwa kuanza kuchukua hatua sahihi za kujitibu.

Wanasaikolojia wanaamini kuwa kujua tatizo ni njia sahihi ya kulitafutia ufumbuzi hata kama hakuna ufumbuzi wa kudumu kuhusu suala husika.

Baada ya kupima

Wanasaikolojia wanasema mtu akishapima afya yake na kujitambua, ni rahisi kushawishi hata wengine kufanua hivyo.

“Lakini wapo ambao huwa wepesi kwenda kupima lakini kwenye kupokea majibu ni shughuli.”

Japo inaweza kukuchukua muda kukubaliabna na hali hiyo kutokana na uasili wa binadamu hususan katika kupokea taarifa za kushtua, lakini ni jambo zuri kuhakikisha unaikabili hofu na kupata ukweli kuhusu afya yako.

Wasemavyo wataalamu wa afya Anaeleza Daktari Stanley Binagi wa hospitali ya Amana kuwa kupima afya hakumaanishi mtu huyo anaweza kufa leo. Pia anasema mtu kwenda kupima afya yake haimaanishi kuwa atakutwa na virusi vya Ukimwi la, la hasha.

Dk Binagi anasema kupima ni njia mwafaka ya kusaidia kujua mwenendo wa afya ya mtu kwa ujumla.

Anasema na hata wale wanakutwa na maambukizi ya virusi, inasaidia kujua viko katika hatua gani ili aanze kupatiwa matibabu.

“Kupima kunaweza kumsadia muathirika na watu wanaomzunguka hasa kama yuko katika uhusiano na mtu mwingine au kwenye ndo,” anafafanua daktari huyo.

Anasema watu wasiogope kujitokeza kupima afya zao kila mara kwani itamsaidia hata kubaini matatizo mengine ya kiafya kama anayo.

Lakini pia kwa wale ambao wanawapenzi, itawasaidia kuwakinga wapenzi wao kwani wataweza kutumia kinga.

“Hii ni kama ilivyo dozi, ili iweze kutibu ugonjwa lazima itumike kwa kiwango stahili. Sasa ukiwa na virusi vichache mwilini unaweza kuwapiga na kinga za mwili ukawa sawa.” anasema.

Hakuna sababu ya watu kuwa na hofu kuhusu kupima afya zao kwani mtu akishajitambua mapema, pia ni kinga kwake.

Kwasababu inamuwezesha kuishi miaka hata 30 na zaidi kwa kujua tu ukweli wa afya yake.

Anasema lazima muathirike atambue hakuna binadamu aliye na uhakika wa kuishi zaidi ya siku moja, kwani katika maisha kifo kipo kila mahali na wakati wowote kinaweza kikatokea. Hivyo kupima na kujua afya yako ni miongoni mwa mambo muhimu kwa mtu kuyaamua.

Dk Binagi anasema hakuna sehemu ilioandikwa mtu atakufa lini, bali ni Mungu pekee ndiye mwenye siri hiyo.

Hivyo, mtu anaweza kukumbwa na mauti kwa sababu mbalimbali, ikiwano kuugua shinikizo la damu, kisukari, moyo na maradhi mengine ambayo kama yangegubdulika mapema, huenda yangetibiwa na mtu akajiongezea siku za kuishi.

Binagi anaongeza kuwa kwa waathirika wa Ukimwi hawapaswi kuwa na hofu, kwani hali imebadilika.

Anasema mtu akishabainika kuwa anamaambukizi ya virusi, madaktari humuanzishia tiba mara oja, tofauti na awali, ilipokuwa inasubiriwa hadi kinga zake za mwili za mwili kushuka.

Anasema matibabu hayo yamewasaidia wengi kuendelea kuishi wakiwa na afya njema.

Asemavyo mwanasaikolojia

Mwanasaikolojia kutoka Taasisi ya Christom Solution, Charles Nduku anasema hofu ya kupima inasababishwa na ukosefu wa elimu juu ya kujikinga na madhara ya virusi vya Ukimwi na Ukimwi.

Anasema licha ya Serikali na wadau mbalimbali wa afya kuendelea kutoa elimu hiyo nchini, lakini inaonekana bado haijajitosheleza.

Nduku anasema kama elimu ingekuwa imetolkewa kwa kiwango kikubwa, watu wasingekuwa na hofu ya kupima afya zao.

“Hali hii inatukumbusha kuwa bado hatujafika lengo la kuwashawishi Watanzania watambue umuhimu wa kupima afya zao, tuongeze juhudi,” anasema Nduku.

Hata hivyo anasema; kuishinda hofu ya kupima na kujua afya yako, ni miongoni mwa mambo muhimu katika maisha japo kumekuwa na hofu kubwa kuhusu suala hilo.

Anasema Watanzania wakumbuke ni heri nusu shari kuliko shari kamili, waondoe hofu, wajitokeze kwa wingi kwenda kupima afya zao bila kusubiri shuruti.