Unaweza kuepuka, kutibu meno kuwa rangi ya kahawia

Muktasari:

  • Meno yaliyoharibika rangi humuathiri mhusika kisaikolojia. kwa mfano anaweza kujishtukia wakati wa kuzungumza. Hali hii husababisha kutojiamini anapokuwa na watu wenye meno meupe walau kuliko yeye katika shughuli mbalimbali.

Kwa kawaida, meno hutakiwa kuwa meupe lakini kutokana na sababu mbalimbali huweza kuwa na rangi nyingine.

Meno yaliyoharibika rangi humuathiri mhusika kisaikolojia. kwa mfano anaweza kujishtukia wakati wa kuzungumza. Hali hii husababisha kutojiamini anapokuwa na watu wenye meno meupe walau kuliko yeye katika shughuli mbalimbali.

Kwakuwa rangi ya meno itokanayo na kuzidi kwa madini ya floridi huwa haitoki kwa kupiga mswaki, wengi wa waathirika hudhani meno yao ni machafu hata baada ya kupiga mswaki

Hali hii ni matokeo ya tatizo linalotokea kwenye tabaka la nje la meno wakati wa utengenezwaji wa meno husika linalosababishwa na kuwapo kwa kiasi kikubwa cha madini ya floridi kuliko kiwango kinachohitajika.

Hali hii husababisha tabaka la nje la jino lililoathirika kuwa na madini mengine kwa kiwango kidogo wakati madini ya floridi yakiwa mengi kupita kiasi huku tabaka hilo likiwa na vitundu vidogo vidogo (porosity). Hivyo kuyafanya yasiweze kusafishika kwa kupiga mswaki.

Ukubwa wa tatizo hili kwa muhusika hutegemea vitu vingi kama vile umri ambao muathirika amekumbwa na madini hayo kwa wingi au namna mwili wake unavyoyapokea madini hayo. Sababu nyingine ni ukuaji wa mifupa, hali ya lishe kwa ujumla na matatizo ya figo.

Wakati tatizo la kuzidi kwa madini ya floridi huathiri mifupa yote mwilini, athari zinazotokea kwenye meno ya ukubwani ndio changamoto inayopewa kipaumbele zaidi na watu wengi kwani huathiri muonekano wao mzuri wa muhusika hivyo kumnyima uhuru sehemu nyingi anazokuwapo.

Maambukizi

Izingatiwe, kuzidi kwa madini ya floridi kupita kiasi kwenye meno huanza kwa watoto wakiwa wadogo wenye miezi 20 mpaka 30. Halikadhalika ni muhimu kujua kuwa umri mpaka miaka minne ya mtoto bado anakuwa katika kipindi hatarishi cha kuwa na meno yaliyoathiriwa na madini haya katika utu uzima wake. Hata hivyo kuanzia miaka minane na kuendelea, mtoto hawezi kuathirika tena.

Kiwango salama cha madini ya floridi kwa binadamu ni 0.05 to 0.07 mg F/Kg/kwa siku. Kiasi chochote juu ya kiwango hiki husababisha kuongezeka kwa uwezekano wa kuwa na meno yaliyoathirika.

Athari za kuzidi kwa madini ya floridi hivyo kuathiri rangi ya meno zinaweza kuepukwa kwa kudhibiti kiasi cha madini ya floridi ambayo mtoto anapewa mpaka umri usiopungua miaka sita.

Vyanzo vya floridi

Madini ya floridi hupatikana kwa wingi, japo kwa uchache, kwenye maji tunayotumia kwa shughuli mbalimbali kama vile kunywa au kupikia, magadi ambayo hutumia wakati wa kupika vyakula mbalimbali kama vile mrenda na maandazi au kwenye dawa za meno tunazotumia kupigia mswaki.

Madini ya floridi ni maarufu na hujulikana sana kwa uwezo wake wa kuzuia meno kutoboka. Kwa ujumla, madini haya husaidia sana kuimarisha mifupa yote katika mwili wa mwanadamu. Umuhimu wake huonekana zaidi linapokuja suala la uimara wa meno.

Utengenezwaji wa meno, kwa kiasi kikubwa, huhusisha muunganiko wa madini ya phosphorus na calcium ambapo kuongezeka kwa madini ya floridi hufanya muunganiko huo kuwa mgumu zaidi kuweza kuhimili shughuli zote zifanywazo na meno.

Kwa lugha nyepesi, kutokuwepo kwa madini haya mwilini huyafanya meno kuwa dhaifu kiasi cha kushindwa kutafuna, kung’ata au kingine chochote kinachoweza kufanywa na meno.

Madhara ya floridi

Kila kitu ikizidi mahali kinapopaswa kutumika huwa kunakuwa na madhara yanayojitokeza. Hata kuzidi kwa madini ya floridi kwenye meno nako kuna matokeo kam ahayo kutegemea wingi wa madini yaliyozidi.

Kwa kutambua kigezo hicho, tunaweza kwa ajili ya kueleweka kuyagawa katika makundi kulingana na mtazamo wa muhusika na jamii kwa ujumla.

Madhara kidogo. Kundi hili lina watu ambao meno yao yana weupe wa chaki. Hii inaweza kujitokeza kwa jino zima au sehemu ya jino, huenda ikawa kinywa kizima.

Wapo wenye madhara ya wastani. Hii ni kwa ile hali ambayo meno huwa na rangi ya kahawia kwa mbali. Hii husababisha aibu kwa baadhi ya wenye tatizo hilo kiasi cha kuwa wahanga wa kujihisi wenye kasoro kwenye jamii.

Baadhi ya waathirika huwekwa kwenye kundi la wenye madhara makubwa kwa kuwa ni watu ambao meno yao huweza kuvunjika ama kukatika hivyo kuwafanya wapate ganzi ama meno husika kuwa yanauma wakati wa kula ama kunywa. Mara nyingi kundi hili ndilo ambalo wengi wao, meno yao huvunjika vunjika na kutokuwa na sura nzuri. Hawa wanahitaji kuwa makini zaidi ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na kuvunjika au kukatika kwa meno yao.

Namna ya kuzuia hali hii ni kuepuka kutumia maji na vitu vingine vinavyoingiza mwilini ambavyo vina kiwango kikubwa cha madini ya floridi hasa kipindi cha utotoni ambapo meno huwa yanaota.

Ikumbukwe kwamba katika umri wa miezi 20 mpaka miezi 30 tangu mtoto kuzaliwa ndicho kipindi hatari zaidi kinachosababisha hali hii kama mtoto atalishwa vitu vyenye madini mengi ya floridi.