Serikali yaifutia TTCL deni la Sh76 bilioni

Muktasari:

  • Kwa mamlaka aliyonayo chini ya kifungu cha 5(3) na 9 cha Sheria ya Fedha, Waziri wa fedha na mipango, Dk Philip Mpango alibadilisha deni hilo kuwa mtaji Agosti.

Dar es Salaam. Wakati kampuni zote zikitakiwa kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE), Serikali imeifutia deni la Sh76 bilioni Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) na kuligeuza mtaji ili iweze kuimarisha uwezo na kutekeleza majukumu yake kwa ushindani.

Kwa mamlaka aliyonayo chini ya kifungu cha 5(3) na 9 cha Sheria ya Fedha, Waziri wa fedha na mipango, Dk Philip Mpango alibadilisha deni hilo kuwa mtaji Agosti.

Taarifa iliyotolewa na Msajili wa Hazina, Dk Oswald Mashindano inasema lengo la kugeuza mkopo huo kuwa mtaji ni kuitaka TTCL kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, tija na weledi ili kuongeza ushindani katika soko.

Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (Epoca) ya mwaka 2010 inazitaka kampuni zote za mawasiliano kujiorodhesha DSE. Mwisho wa kufanya hivyo ilikuwa Juni, lakini ni Vodacom pekee iliyokamilisha agizo hilo huku nyingine zikiwa bado.