Tigo yafungua duka, wateja kuzawadiwa vifaa vya shule

       Meneja wa huduma kwa wateja wa Tigo Kanda ya Ziwa, Beatrice Kinabo     

Muktasari:

Akifungua duka hilo mwishoni mwa wiki iliyopita, meneja wa huduma kwa wateja wa Tigo Kanda ya Ziwa, Beatrice Kinabo alisema kampuni hiyo inalenga kufungua maduka sita ya kisasa kwenye kanda hiyo ili yafike 15 na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi.

       Sengerema. Katika kuboresha huduma, kampuni ya Tigo imezindua duka la kisasa mjini hapa litakalohudumia zaidi ya wateja 600,000 wa Sengerema sambamba na zawadi za vifaa vya shule.

Akifungua duka hilo mwishoni mwa wiki iliyopita, meneja wa huduma kwa wateja wa Tigo Kanda ya Ziwa, Beatrice Kinabo alisema kampuni hiyo inalenga kufungua maduka sita ya kisasa kwenye kanda hiyo ili yafike 15 na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi.

“Maduka yetu ni ya kisasa na yana kaunta nyingi zaidi za kuhudumia wateja pamoja na sehemu ya kujaribia bidhaa na huduma,” alisema Kinabo.

Katibu tawala wa halmashauri hiyo, Alan Augustine alisema duka hilo ni fursa kwa wakazi wa Sengerema kupata huduma za mtandao na huduma mbalimbali zitolewazo na Tigo kwa ukaribu zaidi.

“Wateja wa Tigo Sengerema wamerahisishiwa, sasa hivi hawatalazimika kwenda umbali mrefu kufuata huduma za mtandao,” alisema Augustine.

Kuwapa ushiriki mkubwa zaidi wananchi wa Sengerema, Tigo imezindua kampeni ya ‘back to school’ mahsusi kwa wateja wa Kanda ya Ziwa watakaopata nafasi ya kujishindia zawadi mbalimbali za shule kila watakapotumia huduma zinazopatikana katika maduka hayo.

Watakaozawadiwa ni pamoja na watakaonunua laini mpya, kurudisha laini iliyopotea, kununua simu ya kisasa aina ya Tecno S1 na R6 na kujiunga na huduma za Tigo za malipo ya baada.