Wapinzani wamkumbuka Kikwete

Muktasari:

Akizungumza ofisini kwake jijini Dar es Salaam, amesema “Ninamkumbuka Kikwete. Ninaposema kwamba ninamkumbuka sikumbuki udhaifu wa Serikali yake, siikumbuki Serikali yake ..... Na tumemsema sana.

Dar es Salaam.  Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu amesema wanamkumbuka Rais mstaafu Jakaya Kikwete kwa namna utawala wake ulivyowaruhusu kufanya siasa bila kubughudhiwa.

Akizungumza ofisini kwake jijini Dar es Salaam, amesema “Ninamkumbuka Kikwete. Ninaposema kwamba ninamkumbuka sikumbuki udhaifu wa Serikali yake, siikumbuki Serikali yake ..... Na tumemsema sana. Tulisema huyu rais ni dhaifu na mimi nilimwandika kwenye orodha ya mafisadi.”

Katika utawala wake wa miaka 10, Rais mstaafu Kikwete alikebehiwa ndani na nje ya Bunge kwa kuitwa rais dhaifu, lakini miezi 10 tu tangu astaafu, wapinzani wake wa kisiasa wameanza kumkumbuka.

Kikwete, ambaye alistaafu urais baada ya Rais John Magufuli kuapishwa Novemba 5, 2015, anakumbukwa na wapinzani kwa namna utawala wake ulivyoongeza kasi ya kukua demokrasia na kuukuza upinzani.