Mtukufu Aga Khan kuteta na Rais Magufuli

Muktasari:

Mtukufu Aga Khan baadaye atakuwa na mazungumzo na Rais John Magufuli.

Dar es Salaam. Kiongozi wa madhehebu ya Shia Ismailia duniani, Mtukufu Aga Khan amewasili nchini kwa mwaliko wa Rais John Magufuli.

Mtukufu Aga Khan amewasili leo Jumatano saa nne asubuhi na amepokewa na viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa,  Dk Hussein Mwinyi na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako.

Baada ya kushuka kwenye ndege, Mtukufu Aga Khan alikagua gwaride lililoandaliwa na Jeshi la Polisi na kutazama burudani ya vikundi vya ngoma.

Kiongozi huyo atakuwa na mazungumzo na Rais Magufuli baadaye mchana na kesho atahitimisha ziara nchini.

Mtukufu Aga Khan pia ni kiongozi mwasisi wa Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan ambao unatoa huduma mbalimbali duniani.

Kwa Tanzania mtandao huo unatoa huduma za afya, bima, elimu, mikopo kwa wajasiriamali, kusaidia kilimo na hasa kwa wakulima wa vijijini.

Ziara ya Mtukufu Aga Khan inalenga kuimarisha ushirikiano baina ya Serikali na taasisi yake ambayo ina uwekezaji mkubwa nchini.