Binti adaiwa kutoa mimba, akamatwa

Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa

Muktasari:

Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa amesema jana kuwa mwanafunzi huyo na mshirika wake wanatarajiwa kufikishwa mahakamani upelelezi ukikamilika.

Moshi. Mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Matala wilayani hapa amekamatwa na polisi kwa madai ya kutoa mimba.

Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa amesema jana kuwa mwanafunzi huyo na mshirika wake wanatarajiwa kufikishwa mahakamani upelelezi ukikamilika.

“Tunamsaka kijana aliyempa mimba na atakapopatikana sheria itafuata mkondo kwa kumfikisha mahakamani,” amesema.

Mbali na mwanafunzi huyo aliyelazwa Hospitali ya Kilema, pia jeshi hilo linamshikilia mama yake mdogo kwa madai ya kumsaidia kutekeleza kitendo hicho.

Babu wa mwanafunzi aliyetoa mimba, Henry Kaale amelalamika kushikiliwa kwa wanafamilia wakati mtuhumiwa muhimu hajakamatwa.