Bobi Wine kufikishwa mahakamani Alhamisi

Muktasari:

Mpaka sasa Bobi Wine anashikiliwa kwenye gereza la Makindye ambalo ni la kijeshi huku akiwa hawezi kutembea wala kuzungumza.


Kampala,Uganda. Mbunge wa Kyandondo Mashariki Robert Kyagulanyi 'Bobi Wine' anatarajiwa kufikishwa katika Mahakama ya Kijeshi kwa kumiliki silaha kinyume cha sheria.

Mpaka sasa Bobi Wine anashikiliwa kwenye gereza la Makindye ambalo ni la kijeshi huku akiwa hawezi kutembea wala kuzungumza.

Wiki iliyopita Bobi Wine 32, na watu wengine walishtakiwa baada ya kampeni za kuelekea uchaguzi mdogo eneo la Arua kaskazini mwa nchi. Polisi wanasema walikuwa wamewaongoza wafuasi wao kushambulia msafara wa Rais  Yoweri Museveni.

Mwanasheria wa mbunge huyo  Male Mabirizi amefungua kesi Mahakama Kuu kutaka kuachiwa kwa mbunge huyo na wenzake wakiwamo na wanaharakati mbalimbali waliokamatwa kwenye tukio hilo.

Mwanasheria huyo alisema kwamba  wine amechomwa sindano yenye dawa ambayo inamfanya asijitambue na mpaka sasa hajitambui wala uso wake hautambuliki masikio, pua zinatoa damu.

 Alisema daktari wa jeshi anadanganya  kwamba sindano waliyomchoma ni ya kupunguza maumivu ya kupigwa lakini sio kweli.

Mwanasheria huyo alisema kwamba madai ya kwamba Bobi Wine alikamatwa akiwa na silaha sio kweli kwa sababu alienda mpaka kwenye hoteli na kuzungumza na mmiliki akamwambia kwamba hajawahi kumuona akiwa na silaha yoyote.

Alisema mmiliki huyo alimpa utaratibu wa hoteli yake kwamba ni lazima wakague kila anayeingia ndani na hawajawahi kumuona akiwa na silaha na hata kamera zinaonyesha kwamba hakuwa na silaha.

Alisema aliambiwa na mmiliki wa hoteli hiyo kwamba baada ya kukamatwa Bob wine, wanajeshi sita waliingia  hotelini hapo huku wakikataa  kukaguliwa wakati wa kuingia.

 

.