Dk Shein aanza ziara ya wiki moja Falme za Kiarabu

Muktasari:

Akiwa mjini Abu Dhabi,  atakutana na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Abudhabi, Mohamed Saif Suwaid

Dar es salaam. Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein ameondoka leo kwenda nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kwa ziara ya wiki moja kufuatia mwaliko wa viongozi wa mataifa hayo.

Taarifa iliyotolewa leo Januari 20,2018  na Ikulu ya Zanzibar inaeleza kuwa katika ziara hiyo inayotarajiwa kuanza kesho,  Dk. Shein atafanya mazungumzo na Mtukufu Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, mrithi wa mtawala wa Abu Dhabi na Naibu Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi vya (UAE) nchini Abu Dhabi.

Akiwa mjini Abu Dhabi,  atakutana na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Abudhabi, Mohamed Saif Suwaid, atatembelea mji wa nishati, Masdar, atatembelea jumba la kumbukumbula Louvre, msikiti wa Shaikh Zayed na sehemu ya kihistoria ya Wahat Al Karama.

 

Aidha, Dk. Shein atafanya ziara Dubai na kukutana na kufanya mazungumzo na mtukufu Shaikh Mohammed bin Rashid Al Makhtoum, Makamo wa Rais na Waziri Mkuu wa (UAE) na mtawala wa Dubai.

Katika nchi hizo za Umoja wa Falme za Kiarabu, Pia  Dk Shein atafanya ziara mjini Sharjah na kukutana pamoja na kufanya mazungumzo na Mtukufu Dk. Shaikh Sultan Mohammed Al Qasimi, Mtawala wa Sharjah.

Katika ziara hiyo, Dk. Shein ameongoza na viongozi mbali mbali akiwemo mke wa Rais wa Zanzibar, Mwanamwema Shein, Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Khalid Salum Mohamed, Waziri Asiyekuwa na Wizara Maalum Juma Ali Khatib,pamoja na Mshauri wa Rais Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Uchumi na Uwekezaji Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa.