Fujo zamlazimisha Spika kuahirisha Bunge
Muktasari:
- Fujo zilianza baada ya utaratibu wa kuwasilisha hoja bungeni kukiukwa
- Kutokana na Spika wa Bunge kuelemewa na fujo hizo aliamua kuahirisha
- Baada ya kuahirishwa wabunge wa upinzani walilipuka kwa shangwe
Spika Rebecca Kadaga jana alilazimika kuahirisha Bunge saa nane mchana baada ya wabunge wa upinzani kumvuruga Mbunge wa Igara Magharibi, Raphael Magezi hadi akashindwa kuwasilisha hoja ya kufuta ukomo wa umri wa rais.
Kwa mara ya pili katika muda wa siku tano, wabunge hao walisimama na kuanza kuimba kwa zaidi ya dakika 20 ndani ya Bunge katika juhudi zao za kuzuia pendekezo hilo ambalo Spika alipanga liwasilishwe asubuhi.
Spika Kadaga hakusikilizwa tena kwani kila alipowataka wabunge kutulia ili shughuli ziendelee alipuuzwa na wabunge hao waliokuwa wamejawa hasira huku wakiimba mfululizo Wimbo wa Taifa wa Uganda.
"Bunge limeahirishwa hadi saa 8.00 mchana kesho (leo)," alisema Kadaga huku wabunge wa upinzani wakishangilia kwa shangwe.
Mapema asubuhi Spika Kadaga alimpa Magyezi nafasi ya kuwasilisha hoja ya kutaka Bunge lifanye marekebisho kwa kuifuta Ibara ya 102 (b) katika Katiba ili kuondoa ukomo wa umri wa rais.
Kizaazaa kingine jioni
Saa 1:05 jioni, baada ya Bunge kukamilisha taratibu zote za mchana kama zilivyopangwa katika Ratiba ya Shughuli za Bunge, Katibu wa Bunge, Jane Kibirige alitoa fursa kuwasilishwa kwa hoja inayoliomba Bunge kuandaa na kuwasilisha muswada binafsi unaotaka uondolewe ukomo wa umri wa rais kutoka miaka 75 sasa.
Lakini Mwanasheria Mkuu Kivuli Medard Lubega Sseggona alitaka utaratibu uzingatiwe kwani aliyewasilisha hoja kwanza alikuwa Mbunge wa Kassanda Kaskazini Patrick Nsamba hivyo akataka ijadiliwe hiyo kwanza.
"Tuna wasiwasi kwamba mnavurugwa na watu ambao wanataka shughuli zao zifanyike kwanza,” alisema Sseggona. Mbinu za ucheleweshwaji zilianza pale Mbunge wa Manispaa ya Ntungamo Gerald Karuhanga aliposimama na kuanza kusoma Katiba bila kueleza kama lilikuwa suala la utaratibu au la.
Spika Kadaga, hata hivyo, alisema suala hilo liliibuliwa wakati yeye akiwa nje ya nchi na kwamba naibu wake Jacob Oulanyah, aliamua kwamba hoja hiyo iwasilishwe na kujadiliwa kwa wakati mwafaka. Kadaga alisema hoja zote zitapangiwa muda lakini miswada itapewa kipaumbele.
Mbunge wa Kaunti ya Lwemiyaga Theodore Ssekikubo alimpinga Spika Kadaga akisema kuwa hadi wakati huo hakukuwa na mswada wowote isipokuwa hoja.
Fujo zilizuka upya ndani ya Bunge baada ya wabunge wa upinzani kuibua masuala ya taratibu na kanuni. Walivaa kila mmoja utepe mwekundu na wakasimama licha ya ukweli kwamba tayari Spika Kadaga alishaamua awali kwamba itaondolewa.