Hospitali Serikali majanga matupu

Wagonjwa wakiwa wamelazwa chini kwenye wodi ya Sewaaji, katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam jana. Picha na Anthony Siame

Muktasari:

Hata hivyo, mgonjwa huyo ambaye alikuwa akikohoa mfululizo kiasi cha kutapika, hakuweza kununua dozi hiyo kwani hakuwa na fedha hivyo kurudi wodini kuendelea kukaa akisubiri siku dawa zitakapofika au kupata fedha.

Dar na Mikoani. Hakufai. Pengine ni neno linaloweza kuwakilisha uhalisi wa hali ilivyo katika baadhi ya hospitali kadhaa za Serikali nchini, ambako mamia ya wagonjwa wanateseka kutokana na uhaba wa dawa, vitendanishi na vifaa tiba ambao umeendelea kuzikumba.

Wengi wa wagonjwa waliohojiwa wanalalamikia kushindwa kumudu gharama za dawa ambazo wanapaswa kuzinunua kwenye maduka wakisema hali hiyo inazifanya afya za Watanzania wengi wenye kipato cha chini wanaozitegemea kuwa shakani.

Gazeti hili katika uchunguzi wake limebaini kuwa, uhaba huo pia umesababisha

hospitali nyingi kuwabana wagonjwa kwa kuwatoza fedha kwa ajili ya huduma, ili kujijengea uwezo wa kununua dawa chache, pamoja na vifaa tiba kwa ajili ya dharura.

Kwa jumla, hali ilivyo ni tofauti ya matarajio ya wengi kwamba kungekuwa na mabadiliko, hasa baada ya Serikali kutangaza kwamba imekwishalipa sehemu kubwa ya deni ililokuwa ikidaiwa na Bohari Kuu ya Dawa (MSD).

Hivi karibuni Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid alisema wizara yake imeilipa MSD Sh20 bilioni ili kupunguza makali ya uhaba wa dawa. MSD inaidai wizara hiyo zaidi ya Sh90bilioni za ununuzi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi.

Jana, Msemaji wa Wizara ya Afya, Nsachris Mwamwaja alisema: “Siwezi kuzungumza chochote kwa sababu tayari waziri wangu alishatoa tamko bungeni, kwa hiyo kauli yetu ndiyo hiyohiyo aliyotoa mheshimiwa waziri.”

Sura halisi ya uhaba wa dawa inaonekana katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI) na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambako hali imeendelea kuwa mbaya kwani ukosefu huo wa dawa umesababisha baadhi ya wagonjwa kuzidiwa na wengine kupoteza maisha kwa kushindwa kumudu gharama za matibabu.

Hospitalini Ocean Road, mwandishi wetu alikutana na mkazi wa Arusha, Ashura Iddi aliyefika kutibiwa na kufuatana naye hadi katika duka alikokwenda kununua dawa alizoandikiwa.

Akisaidiwa na mwandishi huyo, Ashura ambaye amekatwa mkono wake wa kushoto kutokana na saratani ya mkono iliyosambaa hadi kifuani, aliambiwa na mfamasia katika Duka la Biomed lililo karibu na ORCI kuwa dawa zake za mionzi zinagharimu Sh166,000.

Hata hivyo, mgonjwa huyo ambaye alikuwa akikohoa mfululizo kiasi cha kutapika, hakuweza kununua dozi hiyo kwani hakuwa na fedha hivyo kurudi wodini kuendelea kukaa akisubiri siku dawa zitakapofika au kupata fedha.

Ashura amelazwa ORCI tangu Oktoba 27, mwaka huu na anasema hajapata matibabu zaidi ya kupewa dawa za maumivu aina ya diclofenac. “Nimekosa hata dawa ya allergy (mzio) ambayo inauzwa Sh1,000 nimeambiwa hakuna,” alisema Ashura.

Kaimu Mkurugenzi wa ORCI, Dk Diwani Msemo alisema bado hawajajua iwapo fedha zilizotolewa na Serikali kupunguza makali ya uhaba wa dawa zitasaidia kwa kuwa tatizo ni kubwa.

Mfamasia katika duka la dawa la Biomed, Hilal Shamshudin alisema siku wagonjwa kati ya 20 hadi 50 hufika katika duka hilo kununua dawa za mionzi.

Alisema hata baadhi ya madaktari nao hufika kununua dawa hizo kwa ajili ya wagonjwa ambao pengine huwapa fedha wawasaidie kuzitafuta.

Mfamasia huyo alisema dawa za mionzi ni ghali kwani wapo wagonjwa wenye dozi kubwa ambao hutakiwa kununua dozi ambazo gharama zake ni kati ya Sh3 na 4milioni.

Mwanamke mwingine, Saumu Mfyonsi ambaye alikuwa akisumbuliwa na saratani ya utumbo, alifariki jana kutokana na kukosa dawa.

Ndugu wa Saumu, Abdallah Mfyonsi alisema waliandikiwa dawa za zaidi ya Sh2 milioni lakini wakati wakizitafuta ndugu yao alifariki. “Wote huu ni umaskini,” alisema Mfyonsi huku akibubujikwa na machozi.

 

Neema maduka ya dawa

Maduka mengi ya dawa yaliyojengwa pembezoni mwa hospitali hizo za umma, yananeemeka kwa kupata wateja wengi ambao kila wanapoandikiwa dawa na madaktari hulazimika kwenda kuzinunua nje ya hospitali husika.

Katika maduka ya dawa yaliyopo mbele ya lango la kuingilia katika Hospitali ya Manispaa ya Temeke, baadhi ya wafamasia wake waliwaambia waandishi wetu kwamba dawa zinazoongoza kwa kuwa na wateja ni zile zinazohusishwa na kina mama wajawazito na uzazi.

Katika orodha ya dawa zinazonunuliwa kwa wingi pia zimo za kutibu malaria, shinikizo la damu na kisukari. “Hapa pia tunauza kwa wingi, vifaa tiba kama mipira kwa wagonjwa waliofanyiwa upasuaji (wa kupitishia mkojo) ambao hutumiwa na wanawake na wanaume,” alisema mmoja wa wafamasia.

Waandishi walishuhudia mwanamume aliyeingia katika duka hilo na kununua mpira wa mkojo wenye urefu wa mita 21, kwa ajili ya mgonjwa wake aliyelazwa wodini.

Wakati hayo yakitokea, uchunguzi wa gazeti hili ulibaini kuwa kuna uhaba mkubwa wa dawa katika hospitali hiyo ya Temeke.

Chanzo chetu ndani ya hospitali hiyo kilisema hali ya dawa ni mbaya na hakuna hata dawa za kutuliza maumivu, hivyo msaada wa haraka unahitajika wakati wakiendelea kusubiri mgawo kutoka MSD.

Chanzo hicho kilieleza kwamba kwa sasa madaktari wanalazimika kuwaandikia wagonjwa dawa ili waende kununua katika maduka yaliyopo nje.

“Kwa sasa stoo yetu ya dawa haina kitu, kiasi kidogo kilichopo kina dawa chache ambazo haziwezi kukidhi mahitaji ya wagonjwa wanaofika hapa. Zaidi, tuna upungufu mkubwa wa vifaatiba muhimu ambavyo pia wagonjwa wanalazimika kwenda kuvinunua nje ya hospitali,” alisema ofisa mmoja ambaye aliomba jina lake lisitajwe.

Alisema dawa muhimu zinazohitajika kwa sasa ni pamoja na amocyllin, ciprofloxcan, diclofenac, diclofenac injection, cannular, misoprosol (kuzuia utokwaji wa damu kwa wajawazito), multivitamin, albendazol na mobendazole.

Baadhi ya vifaa tiba muhimu vilivyopelea ni pamoja na mipira ya kutolea mkojo kwa wagonjwa, (catheter), namba 16 na 18 , kifaa cha kuchomea sindano(cannular), mipira ya mikono na vitendanishi.

Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo, hakuwepo hospitali jana na alipopigiwa simu, iliita bila majibu.

 

Muhimbili majanga

Katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Wodi za Sewa Haji na Kibasila zimefurika wagonjwa hadi kwenye veranda na milango ya wodi hizo kutokana na wagonjwa wanaotokana na ajali.

Msemaji wa Taasisi ya Mifupa ya Hospitali Muhimbili (Moi), Almasy Jumaa alisema zaidi ya asilimia 60 wamepata ajali za bodaboda na bajaji.

“Wodi hizo zina uwezo wa kulaza wagonjwa kwenye vitanda 30 kila moja, lakini sasa idadi ya wagonjwa imekuwa ikiongezeka hadi mara tatu ya uwezo wa wodi na sisi hatuwezi kukataa kuwapokea, kwa hiyo pamoja na matatizo mengine, tunawapokea na kuwalaza ndiyo maana unaona wamejaa kiasi hicho,” alisema Almasy.

Mmoja wa wagonjwa, Elizabeth Biligimana alisema tangu amelazwa na mgonjwa wake katika hospitali hiyo, Aprili mwaka huu kwa ajili ya uchunguzi wa tumbo kujaa, hajawahi kupata dawa za bure.

“Mara nyingi naambiwa ninunue baadhi na baadhi napata huko ndani, ukiniuliza kuhusu kununua dawa naona kama unatonesha vidonda vyangu,” alisema Biligimana.

Almasy alisema japokuwa hawezi kuelezea kwa kina tatizo lililopo, lakini uhaba wa dawa umekuwa kikwazo cha utoaji wa huduma katika viwango vinavyotakiwa kwa kuwa wagonjwa wanalazimika kuandikiwa kutafuta dawa nje ya hospitali.

“Kwa kiasi fulani utaratibu wa uchangiaji ambao wagonjwa wanatakiwa kuchangia huduma ndiyo ambao umekuwa ukitusaidia angalau kupata fedha kidogo kwa ajili ya kupata dawa za kusaidia kunusuru hali,” alisema.

Hata hivyo, kuhusu kiwango cha uhaba na hatua zinazochukuliwa, alisema hawezi kulizungumzia hilo kwa kuwa tayari Waziri wa Afya alishatoa tamko na kueleza kwamba Serikali imeshatoa fedha kwa MSD kwa ajili ya kulipa madeni yake na kusambaza dawa katika hospitali zote za Serikali.

 

Imeandikwa na Florence Majani, Andrew Msechu na Kalunde Jamal