Mahakama yamwacha Ray njia panda kesi ya Lulu

Muktasari:

Ray amesema yeye si mtaalamu wa sheria lakini hukumu hiyo ya Lulu imemgusa

Dar es Salaam. Mwigizaji wa filamu, Vicent Kigosi maarufu Ray amesema uamuzi wa Mahakama dhidi ya msanii mwenzake Elizabeth Michael ‘Lulu’ umemfanya abakie katikati bila kuwa na msimamo wowote.

Ray amesema hatua hiyo inatokana na uwezo wake mdogo wa kutofahamu masuala ya kisheria katika uendeshaji wa kesi ya Lulu hivyo hawezi kusema kama ameonewa au hakustahili kupewa adhabu hiyo.

 

“Mimi nipo neutral (katikati) , sijui lolote na siwezi kujadili hukumu yake kama haki ilitendeka au haikutendeka,” amesema.

Alipotakiwa kutoa maoni yake kama sehemu ya msanii wa tasnia hiyo kwa Lulu kutumikia miaka miwili, Ray amesema  ameguswa na hukumu hiyo.

Amesema ni jambo la kushangaza kuona msanii mwingine akifurahia matatizo aliyokutana nayo Lulu: “Kama binadamu huwezi kuona msanii mwenzako na ukafurahia ni jambo linaloumiza sana,” amesema.