Joti atoa siri ya mkewe kumkubalia kuigiza mwanamke

Msanii wa vichekesho, Lucas Mhavile 'Joti',

Muktasari:

Msanii wa vichekesho Joti amesema hulazimika kumuandaa kisaikolojia mkewe kabla ya kwenda kuigiza 'scene' za mahusiano ili kuepuka kumuudhi.

Msanii wa vichekesho, Lucas Mhavile 'Joti', amesema kwa sasa kuna baadhi ya 'scene' akicheza inabidi amuandae mkewe kisaikolojia.

Akizungumza katika uzinduzi wa msimu wa pili wa vichekesho vya Mwantumu, vitakavyokuwa vikirushwa kupitia chaneli ya DStv Maisha Magic Bongo, Joti amesema scene hizo ni zile zinazohusu mapenzi.

Joti amesema jambo hilo hulifanya kwa kuwa mke wake kama binadamu anaweza akakasirika na hivyo humshirikisha mambo mengi yanayohusu kazi yake.

"Tofauti na zamani, huyu sasa ni mke wangu kila ninachofanya napaswa kumshirikisha kwani kuna baadhi ya sehemu nitatakiwa kuigiza kama mpenzi wa mtu hivyo lazima nimuandae kabla," amesema Joti.

Kuhusu vichekesho vya Mwantumu msimu wa pili amesema wategemee mambo mengi mazuri kwani vimeboreshwa ukilinganisha na awali na kukiri kuwa amejifunza mengi walipokuwa wakipiga picha zake.

Kwa upande wake Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania, Alpha Mria, amesema tangu kuanza kwa msimu wa kwanza wa vichekesho hivyo vya Mwantumu, Oktoba mwaka huu, vimekuwa na msisimko wa aina yake na vimepokelewa vizuri na watazamaji na kuvifanya kuwa na mashabiki wengi.

"Msimu huu mashabiki watashuhudia mikasa ya aina yake ambapo baada ya Bahati kupata ujauzito, baba yake Mzee Mwalubadu anaamua kumpeleka Kaboba katika vyombo vya kisheria," amesema Mria.

Tofauti na awali vichekesho hivyo vilivyokuwa vikirushwa mara moja, sasa hivi vitakuwa vikionyeshwa mara mbili kwa siku ya Jumanne na Jumatano saa 1:30 usiku.