Katambi asema hanunuliki

Muktasari:

Mwenyekiti wa Chadema asema hatishwi kuondoka kwa Katambi kwa sababu chama kina viongozi wengi wenye uwezo wa kukifanya kisimame imara

Dar es Salaam. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi amesema tuhuma zinazoelekezwa kwake kwamba amenunuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) hazina ukweli.

Katambi ambaye jana alitangaza kujiunga na CCM ametoa kauli hiyo kipindi ambacho kumekuwa na tuhuma zinazoelekezwa kwake  ikiwamo ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kwamba ameshawishiwa na akakubali.

Akizungumza na Mwananchi leo Novemba 22, Katambi amesema hakuna mtu yoyote anayeweza kumnunua huku akisema Chadema kimepoteza dira hivyo wenye uelewa wataondoka.

“Nimesikia mengi, nitafanya mkutano na waandishi wa habari, nilidhani wangejitathimini katika ukweli ili kusaidia vijana, chama na taifa lakini kama wanaamua kushambulia mtu kwa uongo bila ushahidi, nitasema ukweli waziwazi,” amesema Katambi

Kuhusu tuhuma za rushwa, Katambi amesema ‘’Katambi hanunuliki wala hana bei naishi katika Principle…kwa wenye akili wangejua dira imepotea watafute upya masafa.”

Awali leo asubuhi, Mbowe ambaye ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni akizungumza  na Mwananchi kuhusu kuondoka kwa Katambi amesema;

"Badala ya nguvu na fedha kuzielekeza kujenga viwanda wao nguvu wamezielekeza kushawishi viongozi wetu, wamewashwishi wengi na Katambi ni miongoni ingawa wengine wamekataa."