Magufuli ataka viongozi wa CCM kutoitwa waheshimiwa

Muktasari:

Kama umewahi kusikia kiongozi wa CCM anaitwa mheshimiwa hakika anapaswa kumsikiliza Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Humphrey Polepole ambaye leo amesema kuwa Rais John Magufuli ameagiza viongozi wote wa chama kutoitwa waheshimiwa, badala yake waitwe ndugu au komrediss

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Rais John Magufuli ameelekeza kuwa ni marufuku kwa kiongozi yeyote wa chama hicho tawala nchini Tanzania kuitwa mheshimiwa, badala yake waitwe ndugu au komredi.

Hayo yameelezwa leo Jumatatu  Januari 7, 2019 na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Humphrey Polepole wakati akihojiwa katika kipindi cha Power Breakfast kilichorushwa na Redio Clouds.

“Nimefarijika kwa jambo moja, mmenitambulisha kama Komredi, kwa Chama cha Mapinduzi viongozi wote kwa sasa hivi mwenyekiti na vikao wameelekeza ni marufuku viongozi wote kuitwa mheshimiwa, wote tunaitwa ndugu au komredi,” amesema Polepole.