Magufuli ataka waliotajwa sakata la tanzanite, almasi wakae pembeni

Rais John Magufuli

Muktasari:

  • Rais Magufuli amesema wateule wake waliotajwa katika ripoti ya kamati hawawezi kuendelea na kazi wakati vyombo vya ulinzi na usalama vikifanya uchunguzi. 

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amewataka wateule wake wote waliotajwa katika ripoti za kamati zilizotathmini mfumo wa uchimbaji, usimamizi, umiliki na udhibiti wa madini ya tanzanite na almasi kukaa pembeni kupisha vyombo vya ulinzi na usalama kufanya kazi zake.

Rais Magufuli amesema hayo leo Septemba 7, Ikulu jijini Dar es Salaam, baada ya kupokea ripoti za kamati hizo zilizoundwa na Spika wa Bunge, Job Ndugai.

Ripoti za kamati hizo zimewataja baadhi ya viongozi wa Serikali akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, James Mdoe; Waziri wa Tamisemi, George Simbachawene na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Edwin Ngonyani.

Awali, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alisema alikuwa na uwezo wa kuwachukulia hatua mawaziri waliotajwa jana Septemba 6 alipokabidhiwa ripoti ya kamati hizo lakini hakufanya hivyo na badala yake aliamua ripoti ziwasilishwe kwa Rais John Magufuli ambaye ni mwanzilishi wa suala hilo ili liwe wazi zaidi.

Waziri Mkuu, Majaliwa amesema alipendekeza ripoti hizo zikabidhiwe kwa Rais Magufuli ili kuendeleza utaratibu wa kuyaweka mambo hayo wazi na kuwaeleza ukweli Watanzania.