Mahakama ‘yaikaba koo’ Pride Tanzania deni la CRDB

Muktasari:

Pride Tanzania ilichukua mkopo kwa jina la Promotion of Rural Initiatives and Development Enterprises Limited na ilikubaliwa ingeulipa na riba ya asilimia 17.

Arusha. Mahakama Kuu imeitaka Pride Tanzania kuilipa Benki ya CRDB zaidi ya Sh12 bilioni zilizotokana na mkopo.

Pride Tanzania ilichukua mkopo kwa jina la Promotion of Rural Initiatives and Development Enterprises Limited na ilikubaliwa ingeulipa na riba ya asilimia 17.

Uamuzi huo ulitolewa Alhamisi wiki iliyopita na Jaji L.J.S Mwandambo wa Mahakama Kuu Kitengo cha Biashara.

Kesi hiyo ilifunguliwa na benki hiyo ikimhusisha aliyekuwa mtendaji mkuu wa taaasisi hiyo, Rashid Malima na Dk William Lyakurwa kwa niaba ya Pride Tanzania. Washtakiwa hao walikutwa na makosa ya kuvunja mkataba uliowawezesha kukopeshwa fedha hizo.

Hivyo mahakama hiyo iliiamuru Pride Tanzania kuilipa CRDB Sh12,050,745,634. Riba ya mkopo huo ambayo ni asilimia 17 itaanza kuhesabiwa tangu siku kesi ilipofunguliwa hadi siku ya hukumu.

Mahakama pia imemtaka mshtakiwa (Malima), kuorodhesha nyaraka za fedha za Pride Tanzania.