Mastaa nane Bongo wasota rumande
Muktasari:
- Mastaa wanane wanashikiliwa na polisi kutokana na matukio
tofauti waliyofanya.
Dar es Salaam. Mastaa wanane wa Bongo wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Tanzania na kila mmoja akiwa na tuhumu yake kutokana na kosa
alilofanya.
Shafii Dauda na Mc Luvanda wanashikiliwa kwa kesi ya kumiliki na
kuendesha blogi bila ya kibali ambacho walitakiwa kulipwa Mamlaka ya
mawasiliano ya Tanzania (TCRA).
Mwingine ambaye anashikiliwa ni Ben Ali (Ben On Air) ambaye alikuwa
muendeshaji wa Dauda TV kupitia mtandao wa (Youtube).
Maua Sama na Soudy Brown wanatuhumiwa kwa kosa la uharibifu wa mali za umma kwani walichapisha video katika mitandao ya kijamii
iliyowaonyesha wakikanyaga pesa za Kitanzania.
Wengine ambao wanashikiliwa ni Tumaini Makene ambaye anaendesha blogu ya Chadema, Fadhili Kondo ambaye ni meneja wa msanii wa kizazi kipya
Maua Sama, meneja wa Shetta Michael Mlingwa (Mx Carter). Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa alisema ana taarifa ya kukamatwa kwa watu hao lakini kama wataongezeka atatoa taarifa rasmi muda utakapofika.
"Katika ofisi yangu yapo hayo majina nane kwa tuhuma za kuendesha
blogu bila ya kuwa na kibali ambacho walitakiwa kulipia ili kuwa na
haki ya kutumia na kuendesha," alisema Mambosasa.