Matumizi ya simu kwa madereva yaundiwa sheria

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Mwigulu Nchemba akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Dk Mwigulu amesema hali ya usalama wa barabarani imeendelea kuimarika kutokana na hatua za kisheria zinazochukiliwa.


Dodoma. Serikali kwa kushirikiana na wadau wameandaa mapendekezo ya Sheria ya Usalama wa Barabarani sura 168 ambapo pamoja na mambo mengine inalenga kuzuia matumizi mabaya ya simu wakati dereva anapoendesha gari.

Akiwasilisha bajeti yake kwa mwaka wa fedha 2018/19, Waziri wa Mambo ya Ndani Dk Mwigulu Nchemba amesema pendekezo jingine ni kuondoa nukta kwenye leseni za madereva wanaokiuka Sheria za usalama wa barabarani.

Dk Mwigulu amesema hali ya usalama wa barabarani imeendelea kuimarika kutokana na hatua za kisheria zinazochukiliwa kwa madereva na wamiliki wa vyombo vya moto.

Amesema katika kipindi cha Julai mwaka 2017 hadi Machi mwaka 2018 jumla ya ajali 4180 za barabarani ziliripotiwa na kwamba ajali 1613 zilisababusha vifo vya watu 1985 na watu 4447 kujeruhiwa.

" Takwimu zinaonyesha kupungua kwa ajali za barabarani kwa asilimia 35.7ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2016/17," amesema.