Mbunge apokea mishahara mitano ya utumishi hewa

Mbunge Makete (CCM), Profesa Norman Sigalla ambaye alikuwa mkuu wa Wilaya ya Songea.

Muktasari:

Wadau walishawahi kueleza kuwa msako wa watumishi hewa uliwahusu wafanyakazi wa kariba ya chini na hivyo kuokoa fedha kidogo, lakini sakata la Profesa Sigalla limeonyesha kuwa hata kariba ya juu serikalini inahusika.

Songea/Dodoma. Sakata la watumishi hewa sasa limefikia pabaya baada ya msako wa watu wanaolipwa fedha bila kuwapo kazini kumkumba Mbunge Makete (CCM), Profesa Norman Sigalla ambaye alikuwa mkuu wa Wilaya ya Songea.

Wadau walishawahi kueleza kuwa msako wa watumishi hewa uliwahusu wafanyakazi wa kariba ya chini na hivyo kuokoa fedha kidogo, lakini sakata la Profesa Sigalla limeonyesha kuwa hata kariba ya juu serikalini inahusika.

Profesa Sigalla anadaiwa kupokea mshahara wa ukuu wa wilaya kwa miezi mitano baada ya kuacha kazi hiyo wakati wa Uchaguzi Mkuu na baadaye kuchaguliwa kuwa mbunge kwa tiketi ya CCM.

Hali hiyo imeisababishia Serikali hasara ya Sh23 milioni.

Baada ya kuacha kazi hiyo ya kuteuliwa na Rais, inadaiwa kuwa Profesa Sigalla aliendelea kupokea mshahara wake wa ukuu wa wilaya wa Sh4.6 milioni kutokana na ofisa utumishi wa ofisi ya katibu tawala wa Mkoa wa Ruvuma kumrudisha kwenye orodha ya malipo ya mshahara.