Mugabe akiri kusafirisha fedha nje ya nchi

Muktasari:

Siri hiyo imefichuliwa na mkewe, Grace Mugabe wakati mumewe alipokutana na waandishi wa habari kwa mahojiano maalumu yaliyofanyika nyumbani kwake wiki iliyopita.


Harare, Zimbabwe. Rais wa zamani wa Zimbabwe, Robert Mugabe amekiri  kutorosha kiwango kikubwa cha fedha nje ya nchi wakati akiwa madarakani, akinunua nyumba mbili, Afrika Kusini na Hong Kong.

Siri hiyo imefichuliwa na mkewe, Grace Mugabe wakati mumewe alipokutana na waandishi wa habari kwa mahojiano maalumu yaliyofanyika nyumbani kwake wiki iliyopita.

Kiongozi huyo wa zamani amewahi kuamuru kutiwa mbaroni aliyekuwa waziri wake wa fedha, Chris Kuruneri aliyetuhumiwa kutorosha fedha nje ya nchi na kununua nyumba ya kifahari Cape Town, Afrika Kusini.

Kwa mujibu wa gazeti moja la Afrika Kusini, Sunday Times, Mugabe ameviarifu vyombo vya Serikali kuhusu ununuzi wa nyumba aliofanya Afrika Kusini na Hong Kong.

“Nchini Afrika Kusini nilinunua nyumba moja iliyochoka na niliitaka nivunje baadhi ya maeneo ili niifanyie ukarabati,” alisema Grace Mugabe.

Pia, alikiri kukodisha nyumba Dubai kwa gharama ya Dola 500,000 za Marekani kwa mwaka kwa ajili ya kijana wao, Robert Mugabe Jr aliyekuwa akisoma nchini humo.

Kuhusu nyumba ya Hong Kong ripoti za vyombo vya habari zinaonyesha, ilinunuliwa mwaka 2009  ikiwa muda mchache kabla ya binti yao, Bona Chikore hajaanza masomo katika Chuo Kikuu cha Hong Kong.