Nape aeleza alichoambiwa na Lissu wakitoka bungeni jana

Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (kulia) akifurahia jambo na mbunge wa Mtama, Nape Nnauye walipokuwa wakitoka kuhudhuria kikao cha Bunge, mjini Dodoma jana mchana.

Muktasari:

  • Nape amesema Lissu alimweleza wanafuatiliwa na alimtaka ahame CCM.

Dodoma. Mbunge wa Mtama (CCM), Nape Nnauye ameeleza alichoambiwa na Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu jana Alhamisi mchana wakati wakitoka bungeni huku wakicheka.

Nape amesema Lissu alimwambia, “Wewe Nape ni mjomba wangu, kwa nini unabaki CCM? Mimi na wewe tunafuatiliwa na jamaa zako wakitumia gari moja. Mimi na wewe ni watuhumiwa, hama CCM mjomba.”

Lissu alipigwa risasi jana Alhamisi mchana na kupelekwa chumba cha upasuaji katika Hospitali ya Rufaa ya Dodoma na baadaye usiku alihamishiwa Hospitali ya Aga Khan ya Nairobi nchini Kenya.

Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini jana wakati Lissu akipelekwa Kenya alisema ameambatana na mkewe, madaktari wawili wasio na mipaka; Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa.

Ndege iliyomsafirisha iliondoka katika Uwanja wa Ndege wa Dodoma saa sita na robo usiku.