Papa ataka kubadili mfumo ili mapadri waoe

Muktasari:

  • Hata hivyo, imefahamika kuwa pengine pendekezo hilo likawaruhusu mapadre wa Brazil pekee kutokana na mjadala unaoendelea nchini humo. Hivi karibuni Askofu wa Brazil, Kadinali Claudio Hummes alimwomba Papa Francis kufikiria kuondoa sheria inayowakataza makasisi kufunga ndoa.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis amependekeza kubadili mfumo wa utumishi wa mapadre akisema itakuwa vyema iwapo makasisi hao wakaruhusiwa kuanza kuoa.

Hata hivyo, imefahamika kuwa pengine pendekezo hilo likawaruhusu mapadre wa Brazil pekee kutokana na mjadala unaoendelea nchini humo. Hivi karibuni Askofu wa Brazil, Kadinali Claudio Hummes alimwomba Papa Francis kufikiria kuondoa sheria inayowakataza makasisi kufunga ndoa.

Ingawa pendekezo hilo la Papa Francis huenda likapunguza tatizo la uhaba wa wanaume wanaojiunga kwenye utumishi huo, lakini linatarajiwa kukabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa waumini wenye msimamo mkali na hata pia kusababisha mgawanyiko ndani ya kanisa.

Ombi hilo linatarajiwa kujadiliwa katika kikao cha baraza la kanisa kinachotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu nchini Brazil.

Kanisa Katoliki linahubiri mafundisho ambayo yanapiga marufuku makasisi wake kufunga ndoa ingawa kumekuwa na baadhi wanaovunja mwiko huo na kuisha maisha ya ndoa. Hata hivyo, wale wanaochukua uamuzi huo hujitenga na kanisa.

Kasisi moja aliyetambulika kwa jina la Paddy O’Kane amenukuliwa na baadhi ya magazeti akielezea uwezekano wa Papa Francis kuchukua uamuzi wa kuwafungulia mapadre kifungo cha kutokua wakati wowote mwezi huu.

“Hivi karibuni nilimsikia Papa anataka kutekeleza ombi alilolipata toka Brazil kama jaribio lake la kwanza,” alisema.

Papa Francis na mtangulizi wake, Benedict XVI wamekuwa wakieleza kuwa suala la makasisi kutoruhusiwa kuoa siyo jambo lisiloweza kubadilika na kwamba jambo hilo linajadilika.