Polisi wazuia mkutano wa Maalim Seif Mtwara

Askari wakiwa nje ya geti la kuingia Stella Maris (Stemmuco) ambako mkutano wa Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad ulitarajiwa kufanyika. (Picha na Haika Kimaro)

Muktasari:

Mkutano huo ulitegemewa kuanza saa 5 asubuhi lakini askari walionekana wakizunguka geti la kuingia chuo cha Stella Maris (Stemmuco) ambako CUF walitegemea kutumia ukumbi wao.

Mtwara. Jeshi la Polisi mkoani Mtwara limeuzuia mkutano wa uliotarajiwa kuhutubiwa leo na Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad.

Mkutano huo ulitegemewa kuanza saa 5 asubuhi lakini askari walionekana wakizunguka geti la kuingia chuo cha Stella Maris (Stemmuco) ambako CUF walitegemea kutumia ukumbi wao.

Katika eneo la chuo hicho yalionekana magari matatu ya askari ambayo pia yalikuwa yakizunguka katika mji wa Mtwara na gari moja la maji ya kuwasha likiwa limesimama kando ya eneo la chuo hicho.

Mkurugenzi wa habari, uenezi na uhusiano wa Umma CUF, Mbarala Maharagande amesema mkutano huo ulilenga kukagua shughuli za chama, kupata maoni ya wanachama pamoja na mapendekezo ya namna ya kuboresha utendaji wa chama kwa ngazi za chini.

Mwandishi wetu aliyeko Mtwara amesema Kamanda wa polisi mkoani humo atazungumza baadaye kuhusu kilichotokea.