Raia wa DRC adaiwa kuiba watoto watatu

Muktasari:

Kamanda wa polisi mkoani Mwanza, Ahmed Msangi alisema kwamba mtuhumiwa huyo alikamatwa Oktoba 18, akiwa katika harakati za kuondoka na watoto hao wanaoishi Mtaa wa Shede, eneo la Mkuyuni.

Mwanza. Jeshi la Polisi mkoani Mwanza linamshikilia raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Ashia Ismail kwa tuhuma za wizi wa watoto watatu Jijini Mwanza.

Kamanda wa polisi mkoani Mwanza, Ahmed Msangi alisema kwamba mtuhumiwa huyo alikamatwa Oktoba 18, akiwa katika harakati za kuondoka na watoto hao wanaoishi Mtaa wa Shede, eneo la Mkuyuni.

“Wakati wa tukio, watoto hao walikuwa wakicheza nje ya nyumba yao,” alisema kamanda Msangi

Alifafanua kwamba baada ya kuwafikia watoto hao, mtuhumiwa alimchukua na kumbeba mgongoni mtoto mdogo huku akiwashikilia mikono wengine wawili na kuanza kuondoka nao kabla ya wakazi wa eneo hilo kumtilia shaka na kutoa taarifa kwa wazazi.

Akizungumzia tukio hilo, mzazi wa mmoja wa watoto hao, Elizabeth Marco alisema kwamba familia yake imeingiwa hofu kuhusu usalama wa watoto wao.

Tukio la kuibwa kwa watoto hao limetokea huku Watanzania wakiwa bado wana kumbukumbu ya matukio ya kusikitisha ya wizi wa watoto yaliyolikumba jiji la Arusha.