Saruji ya Dangote yaadimika sokoni

Muktasari:

  • Wakizungumza jana kwenye mkutano wao na Mkurugenzi wa mauzo na ufundi wa Kampuni ya Dangote group, Johnson Olaniyi waliitaka kampuni hivyo kudhibiti changamoto zinazosababisha hali hiyo.

Dar es Salaam. Wafanyabiashara wa vifaa vya ujenzi jijini hapa wamelalamika kukosekana kwa uhakika wa upatikanaji wa saruji ya Dangote, hivyo kuwasababishia usumbufu.

Wakizungumza jana kwenye mkutano wao na Mkurugenzi wa mauzo na ufundi wa Kampuni ya Dangote group, Johnson Olaniyi waliitaka kampuni hivyo kudhibiti changamoto zinazosababisha hali hiyo.

Mkurugenzi wa G&E investmenta, Goodluk Lyatuu alisema huwa wanasubiri hata wiki mbili bila kupata saruji hali inayosababisha usumbufu kwa wateja, ikiwamo kuzuia mtaji kuongezeka.

Alisema pia bei imekuwa ikibadilika mara kadhaa, hali inayoyumbisha soko na aliuomba uongozi uchukue hatua ili kuwajengea mazingira mazuri ya biashara hiyo.

Saruji hiyo hadi jana kwa bei ya jumla ya mfuko wa kilo 50 uliuzwa kati ya Sh10,700 na 11,200 na bei ya rejareja ilikuwa kati ya Sh12,000 hadi 12,500.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Olaniyi alisema wanatambua kuna changamoto zinazowakabili hasa kwenye uzalishaji lakini watajitahidi kukabiliana nazo.

“ Ndiyo maana tupo hapa tunazungumza hii ni miongoni wa hatua za kutatua changamoto hizo nimetoka Nigeria hadi chini hapa ili kushughilikia mambo hayo,” alisema.

Mkuu wa mauzo wa Dangote, Felista Masambo alisema changamoto hizo kwa upande mwingine zinatokana na teknolojia mpya ya uzalishaji wanayotumia.