Serikali yafuta tozo tano za Osha

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenister Mhagama.

Muktasari:

Ni zilizokuwa zikitozwa na Wakala wa Uslama na Afya Mahali pa Kazi (Osha), ikiwemo ada ya leseni na ukaguzi iliyokuwa ikitozwa Sh200,000

Dodoma. Serikali imefuta tozo tano zilizokuwa zikitozwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (Osha) lengo likiwa ni kuwapunguzia mzigo waajiri.

Tozo zilizofutwa ni ada ya fomu Sh2,000, ada ya ukubwa wa eneo la kazi ambayo ilikuwa ni kati ya Sh 50,000 hadi Sh1.8 milioni.

Nyingine ni ada ya leseni na ada ya ukaguzi Sh200,000, ada ya vifaa vya kuzimia moto Sh500,000 na siku ya usalama kazini ambayo ilikuwa ikitozwa Sh450,000.

Akizungumza leo Alhamisi Septemba 20, 2018 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenister Mhagama amesema kuondolewa kwa tozo hizo ni agizo la Rais John Magufuli.

Mhagama amesema Osha imepitia mambo mengi ikiwemo kupunguza ratiba za ukaguzi ambazo zimekuwa zikifanyika mara kwa mara hasa katika sekta binafsi.

"Kwa mfano katika sekta binafsi kulikuwa na maumivu makubwa zaidi, yaani huyu anakagua hili, kesho mwingine, keshokutwa tena, sasa haipo hiyo na badala yake vyote vitakaguliwa kwa wakati mmoja, kwani tuna mfumo wa taasisi zote kwenda pamoja," amesema Mhagama.

Akizungumzia ajali zilizotokea mwaka jana, amesema jumla ya ajali 755 ziliripotiwa na kati ya hizo vifo vilikuwa 6 na 749 ni majeruhi.

Sekta ya uzalishaji iliongoza kwa asilimia 87, madini asilimia 7, ujenzi asilimia 4 na sekta nyingine asilimia 2.

Amesema utekelezaji wa punguzo la tozo hizo umeanza mara moja kuanzia yalipoanza mabadiliko ya fedha mwaka wa fedha hivyo akatoa onyo kwa watumishi watakaojihusisha na utozaji.