TCU yafungua dirisha jipya udahili wa wanafunzi

Muktasari:

Akizungumza na wandishi wa habari  Mkurugenzi wa  Udahili na Nyaraka wa TCU Dk Kokuberwa Mollel amesema awamu hiyo ya mwisho itakayodumu kwa siku tatu itaanza  Oktoba 24 hadi Oktoba 26.

Dar es Salaam.Tume ya Vyuo Vikuu nchini TCU imefungua awamu nyingine ya udahili ili kuwapa nafasi wanafunzi ambao hawakuchaguliwa katika awamu zilizopita kutuma maombi upya.

Akizungumza na wandishi wa habari  Mkurugenzi wa  Udahili na Nyaraka wa TCU Dk Kokuberwa Mollel amesema awamu hiyo ya mwisho itakayodumu kwa siku tatu itaanza  Oktoba 24 hadi Oktoba 26.

Amesema udahili huo utahusisha waombaji waliokwisha tuma maombi yao lakini walishindwa kuchaguliwa kutokana na kukosa sifa za kuingia katika kozi walizoomba.

“Awamu hii itawahusu waombaji wenye  sifa za kidato cha sita, stashahada na sifa linganishi . Wengi wao walishindwa kuchaguliwa kutokana ushindani mkubwa katika programu walizoomba, kushindwa kukamilisha taratibu za uombaji na waombaji kukosa sifa kwa kozi walizoomba”amesema .

Kwa mujibu wa Dk Mollel hadi sasa wanafunzi 61590 wameshachaguliwa kujiunga kwenye vyuo mbalimbali na wanafunzi 17717 wenye sifa za kujiunga na vyuo vikuu  bado wapo kwenye mfumo wa uchakataji.