Vijiji 12 wilaya ya Misungwi kupata maji

Muktasari:

Alitoa kauli hiyo  jana Februari 19, 2018 wakati akizungumza na wananchi mara baada ya kuweka jiwe la ujenzi wa mradi huo akiwa katika siku ya tano ya ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza. Mradi huo unatarajiwa kuhudumia vijiji 12. 


Mwanza. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewahakikishia wananchi wa wilaya ya Misungwi Mkoa wa Mwanza kuwa vijiji vyote vitapatiwa huduma ya maji safi kupitia miradi inayotekelezwa katika wilaya hiyo ukiwemo wa Mbarika-Misasi utakaogharimu Sh12.4bilioni.

Alitoa kauli hiyo  jana Februari 19, 2018 wakati akizungumza na wananchi mara baada ya kuweka jiwe la ujenzi wa mradi huo akiwa katika siku ya tano ya ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza. Mradi huo unatarajiwa kuhudumia vijiji 12. 

Vijiji hivyo ni Igenge, Lutalutale, Bugisha, Ngaya, Ikula, Sumbugu, Matale, Kasololo, Isuka, Nduha, Manawa na Misasi ambapo jumla ya wakazi 47,011 wanatarajiwa kunufaika na mradi huo.

Amesema Serikali ya Awamu ya Tano ina mikakati mizuri inayolenga kumaliza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo mbalimbali nchini vikiwemo vijiji vya wilaya ya Misungwi ili kuwawezesha wananchi hasa wanawake kushiriki katika shughuli za maendeleo kuliko kutafuta maji.

Waziri Mkuu amesema Serikali kupitia kampeni ya Rais John Magufuli ya kumtua mama ndoo, itahakikisha wananchi katika maeneo yote nchini wanapata huduma ya maji safi na salama katika umbali usiozidi mita 400 kutoka kwenye makazi yao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Misungwi, Eliud Mwaiteleke amesema mradi huo umegawanyika katika miradi midogo minne ambayo ni Igenge, Mbarika-Ngaya, Ngaya-Matale na Matale-Manawa-Misasi.

Amesema shughulli zilizokamilika ni pamoja na ujenzi wa vituo 48 vya kuchotea maji, matanki mapya manne na moja limekarabatiwa pamoja na mtandao wa mabomba wenye urefu wa kilomita 73,087.

Awali, Waziri Mkuu aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa shule ya Sekondari ya Kata ya Gulumungu katika kijiji cha Nyamayinza, ambapo aliwapongeza wakazi wa kata hiyo kwa uamuzi wa kujenga shule, ambayo itawawezesha watoto wao kupata elimu.