Vodacom yaingia rasmi DSE

Muktasari:

  • Hafla ya uzinduzi rasmi wa kuorodheshwa kwa hisa hizo ulifanyika katika ofisi za DSE na kuhudhuriwa na Waziri wa fedha na mipango Dkt Philip Mpango, pamoja na wadau wengine wa soko la hija na mitaji.

Dar es Salaam. Kampuni ya huduma za simu ya Vodacom leo Jumanne, Agosti 15 imeorodheshwa rasmi katika soko la hisa la Dar es Salaam (DSE), ikiweka sokoni jumla ya hisa zake bilioni 2.2.

Hafla ya uzinduzi rasmi wa kuorodheshwa kwa hisa hizo ulifanyika katika ofisi za DSE na kuhudhuriwa na Waziri wa fedha na mipango Dkt Philip Mpango, pamoja na wadau wengine wa soko la hija na mitaji.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao amesema haikuwa kazi rahisi kufikia hatua hiyo ambayo ni maagizo ya Serikali lakini kutokana na ushirikiano na wadau wengine imewezekana.

“Kazi yangu sasa ni kuendelea kuikuza kampuni ya Vodacom iendelee kuongoza katika utoaji wa huduma nchini ili wabia wetu wapya waweze kunufaika na uwekezaji walioufanya,” anasema Ferrao.

Kwa upande wake Waziri Mpango ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo ameipongeza kampuni ya Vodacom kwa hatua iliyofikia na kutumia nafasi hiyo kuzitaka kampuni nyingine kaharakisha mchakato huo kabla hazijachukuliwa hatua za kisheria.

“Najua kuwa kampuni nyingine bado zipo katika hatua mbali mbali, Nakumbusha kwa misisitizo kuwa kampuni hizo zishirikiane na wataalamu wetu katika tasnia ya soko na mitaji ili kukamilisha maelekezo hayo ya sheria ya ‘EPOCA’,”amesema Mpango

Amesisitiza kuwa “Serikali haitasita kuchukua hatua kali endapo itajiridhisha kuwa kampuni hizo zimezembea kutekeleza Sheria hiyo kwa makusudi”