Kura 266 zaipitisha bajeti ya Sh32trilioni bungeni

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango akimpongeza Naibu wake, Dk Ashatu Kijaji baada ya Bunge kupitisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Kati ya wabunge 348 ni 82 ndio walioikataa bajeti hiyo kwa kura za hapana

Dodoma. Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wameipitisha Bajeti ya Serikali ya mwaka 2018/19 ya Sh32.45 trilioni kwa kura 266 kati ya 348 sawa na asilimia 76.

Katibu wa Bunge, Stephen Kagaigai akitangaza matokeo ya kura leo jioni Juni 26, 2018 amesema jumla ya wabunge waliokuwamo bungeni na kupiga kura walikuwa 348.

“Idadi ya wabunge waliopiga kura 348, wabunge 43 hawakuwepo. Kura za hapana 82 na hakuna kura ambayo haikuamua na kura za ndio ni 266,” amesema Kagaigai

Mara baada ya kauli hiyo, shangwe kutoka kwa wabunge wa CCM ziliibuka huku Spika wa Bunge Job Ndugai akiwashukuru Rais John Magufuli, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Amesema mara baada ya kuondoka Ijumaa, bila shaka mawaziri wataondoka wakiwa wamesheheni maoni ya wabunge na ushauri ambao kimsingi umetoka kwa wananchi.