Nyota Ruvu amvulia kofia Yondani

Dar es Salaam. Emmanuel Martin wa Ruvu Shooting amemtaja beki nguli wa Yanga, Kelvin Yondani kuwa ndiye bora katika Ligi Kuu Tanzania Bara.

Akizungumza jana, Martin alisema licha ya ukongwe wake katika mashindano hayo, Yondani amekuwa mhimili wa Yanga katika safu ya ulinzi.

Mchezaji huyo wa zamani wa Yanga, alitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya ya Yanga kuilaza Ruvu Shooting bao 1-0, juzi.

“Yanga wanaweza kumuona Yondani kama mchezaji wa kawaida sisi washambuliaji ndio tunajua jinsi ambavyo anatibua mipango ya kufunga mabao,” alisema Martin.

Mchezaji huyo aaalisema Yanga inaweza kuyumba kama haitamuandaa beki wa kati kurithi nafasi yake baada ya kustaafu.

Alisema katika mechi ya juzi Yondani alikuwa kikwazo kwa kuwa alikuwa akitibua mipango ya kufunga mabao licha ya kuingia ndani ya eneo la hatari mara kwa mara. Kwa upande wa Khamis Mcha alisema mabeki wa Yanga wapo imara lakini katika ufundi ni mhimili wa Yanga hasa katika safu ya ulinzii.

“Anajua kuifanya kazi yake kikamilifu, si beki ambaye mchezaji unaweza ukamvaa kirahisi anapokuwa mbele yako, umri wake unaenda ndio kwanza naona maarifa yake yanaongeze.

Mchezaji huyo amekuwa katika kiwango bora katika Lgi Kuu Tanzania Bara akicheza pacha na Abdallah Shaibu Ninja au Andrew Vincent ‘Dante’.